2015-02-02 10:27:36

Kongamano kuhusu familia!


Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu ni kati ya wajumbe wakuu watakaoshiriki kwenye Kongamano kuhusu Familia litakalofanyika kwenye Kanisa kuu la Kupashwa Bwana Habari, mjini Nazareth, Jumamosi tarehe 7 Februari, 2015. Kongamano hili linaongozwa na kauli mbiu "Wito na utume wa Familia ndani ya Kanisa na Ulimwengu mamboleo".

Kardinali Baldisseri ataratibu maoni, mawazo, tafakari na tafiti mbali mbali zitakazowasilishwa na wajumbe kama sehemu ya mchango wao wa maandalizi ya hati ya kutendea kazi kwa ajili ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia itakayofanyika mwezi Oktoba hapa mjini Vatican. Viongozi wakuu kutoka Nchi Takatifu wanatarajiwa kushirikisha mawazo na mang'amuzi yao.

Kardinali Baldisseri atakapowasili Nchi Takatifu, Ijumaa tarehe 6 Februari anatarajiwa kukutana na familia, kubariki na hatimaye, kuzindua nyumba mpya ya mapokezi kwa ajili ya familia ambazo zinafanya hija ya maisha ya kiroho kwenye maeneo matakatifu. Kardinali Baldisseri wakati wa kongamano, atawashirikisha wajumbe hatua ambazo zimekwishafikiwa katika mchakato wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia. Jumapili, ataadhimisha Ibada ya Misa kwa kutoa Daraja la Ushemasi na Upadre kwa baadhi ya watawa wanaoishi huko Nchi Takatifu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.