Huyu ni nani? Kuanzia jumapili hii na nyingine 12 zifuatazo, Neno la Mungu litajikita
katika swali hili. Jibu la swali hili tutalipata katika Jumapili ya 24 ambapo Injili
ya Marko inatoa jibu kwa swali hili. Nii katika ufunuo ule wa askari wa kirumi tunapata
jibu – Mk. 15:39 – akida aliyesimama mbele yake, alipoona jinsi alivyokata roho alisema,
hakika, mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu. Yesu – anaingia katika Sinagogi. Kila Sabato
walikuwa wanapata mafundisho, lakini leo fundisho lake ni tofauti – aliwafundisha
kama mtu mwenye mamlaka – Mk. 1:22 maana yake nini kufundisha kwa mamlaka?
Tukilinganisha
mafundisho ya Yesu na walimu wa Sheria twaona tofauti kubwa tatu (3).Tofauti kubwa
ya kwanza ipo katika chanzo cha fundisho lenyewe, yaani fundisho linatoka wapi. Fundisho
la Yesu ni: Fundisho lilitoka moyoni na si kichwani.Lina mwelekeo wa roho mpya na
si sheria tu.
Ni changamoto ya kuwa tayari kuanza upya. Mafundisho ya Yesu
yamejaa uhakika kwa vile anajua anaongea ukweli wenye uzima – angalia Yn. 3: 11 –
amin, amin, nakuambia, twasema tunayoyajua, twashuhudia tuliyoyaona, lakini hampokei
ushuhudu wetu. Mafundisho yake ni ushuhuda wa uhusiano wake na Mungu. Walimu wa Sheria,
chanzo cha mafundisho yao ni sheria.
Tofauti kubwa ya pili kubwa kati ya
mafundisho ya Yesu na yale ya walimu wa Sheria ipo katika maana ya fundisho lenyewe.
Yesu anaangalia thamani ya Sheria na maana yake. Waandishi wa Sheria wanakazia ufafanuzi
wa maneno – m.f. kuhusu sabato – lini sabato yaanza na lini inaisha na kazi ipi ya
kufanya na ipi siyo. Yesu anaelezea mpango kazi wa Mungu. Maana mpya ya Sabato
ni kujiacha kwa ajili ya Mungu ili kufanya kazi ya Mungu – Yn. 5:17 - Yesu akasema,
Baba yangu anaendelea na kazi yake, nami ninafanya vivyo hivyo. Yesu anaponya, siku
ya sabato. Kwa Wayahudi ikawa ni dhambi ya mauti. Sasa kati ya kuacha mgonjwa aendelee
kuteseka, kushika sabato kwa sababu sheria inasema hivyo na kumponya mgonjwa ni ipi
ina maana zaidi?
Hii ndiyo taarifa ya ukombozi ya Kristo, taarifa inayokomboa.
Tofauti nyingine ipo katika ujumbe wenyewe:Ujumbe wa Kristo watualika kubadilika moyoni.
Ujumbe wa walimu wa sheria – wafanya watu wajisikie vibaya, inatisha, kuogofya. Yesu
alipopelekewa yule kipofu – alimponya. Walimu wa sheria – nani aliyetenda dhambi.
Yesu anafundisha na kutibu.Wayahudi wanalaumu na kuona kakufuru.
Ndugu
zangu, huu mtazamo mpya wa Kristo uwe leo changamoto kubwa katika maisha yetu. Ni
vizuri pia tukatumia neno la Mungu siku ya leo kuangalia maisha yetu ya ufuasi. Ni
vizuri kuangalia sheria zetu na sheria au amri za Mungu na kuona tuko wapi au tukoje.
Kama Kristo alivyofanya, tukumbuke kuwa jukumu la kwanza ni kumkomboa mwanadamu na
hali yake mbaya. Hatuna budi kuweka katika matendo kile ambacho tunakiamini katika
imani yetu kama Kristo alivyofanya na alivyotufundisha kuishi.
Masomo yetu
ya leo yanatuita tuiitikie sauti ya Mungu. Katika somo la kwanza – tunaona jinsi
mwandishi anavyotambua mapenzi ya Mungu. Mungu anaahidi Nabii, mtu mpole, msemaji
mwaminifu wa neno, mtu wa imani na mlinzi wa huruma ya Mungu. Ndiyo sisi leo. Sote
tunatakiwa kuwa huyo nabii wa Mungu katika mazingira yetu ya leo. Katika somo la Injili
tunaona kuwa, alipo Yesu, upo ufalme wa wake na wa Baba yake. Hivyo shetani hana nguvu
tena. Uwepo wa Kristo ni uzima mpya na wa milele.