Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumamosi, tarehe 31 Januari 2015
katika maadhimisho ya kumbu kumbu ya Mtakatifu Yohane Bosco, miaka mia mbili tangu
alipozaliwa; Mtakatifu aliyejisadaka kwa ajili ya huduma ya kichungaji na elimu kwa
vijana, amezindua rasmi mwaka wa shughuli za mahakama ya mji wa Vatican kwa Ibada
ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.
Mtakatifu
Yohane Bosco katika mbinu zake za malezi kwa vijana, alijikita zaidi katika kuzuia,
kuunda na kushawishi, akiwaachia vijana kujiweka wazi mbele ya Mwenyezi Mungu, ili
aweze kuwafunda zaidi. Ni mtakatifu ambaye alichota mambo mengi ya maisha na utume
wake kutoka kwa Mtakatifu Francisko wa Sale, akionesha utu, heshima, wajibu na haki
ya kila mtu inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Baba wa wote. Imani kwa Kristo
na Kanisa lake, imekuwa ni chachu ya mabadiliko kwa watu wengi duniani.
Mwaka
wa shughuli za mahakama ni sehemu ya mchakato wa huduma ya ukweli inayojikita katika
mchakato wa elimu, dhamana inayotekelezwa katika shughuli za mahakama zinazopaswa
pia kuwa na mwono wa kiimani kwani sheria ni kwa ajili ya kumsaidia mwanadamu kutenda
mema ili kufikia uzuri; watu wajenge utamaduni wa kuzingatia utawala wa sheria; haki
msingi za binadamu sanjari na haki jamii, huku wakiongozwa na kanuni ya dhahabu.
Watu
wapewe elimu ya kujizuia kutenda mabaya, kwa kujenga utamaduni wa kusikiliza, majadiliano
pamoja na kutakiana mema, ili kujenga raia wema na wenye kuwajibika, watu wanaopenda
na kuheshimu sheria na kutenda haki, bila kujitumbukiza katika hatari ya kutaka kulipiza
kisasi. Ni wajibu wa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inatambua kwanza: utu
na heshima ya binadamu.
Lengo la shughuli za mahakama zinazotekelezwa mjini
Vatican ni kwa ajili ya afya ya mioyo ya waamini inayojikita katika sheria asilia,
sheria za Kanisa pamoja na Injili, yote haya ni kwa ajili ya mafao ya wengi, anasema
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican.
Na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.