2015-01-31 09:04:23

Tunu msingi za maisha ya ndoa na familia!


Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, CEI limehitimisha mkutano wake wa mwanzo wa mwaka kwa kukazia umuhimu wa kuibua mikakati itakayowawezesha vijana kupata fursa za ajira, ili kuweza kuwa na matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.

Maaskofu wanakazia na kuendelea kuhimiza waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujenga na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu sanjari na kukataa utamaduni wa kifo na utandawazi usioguswa na shida pamoja na mahangaiko ya wengine.

Maaskofu wanasema, wataendelea kujadiliana na wadau mbali mbali, ili kuhakikisha kwamba, mafao ya wengi yanapewa kipaumbele cha kwanza. Wamejiwekea mikakati ya utekelezaji wa Waraka wa kichungaji wa Baba Mtakatifu Francisko, Injili ya Furaha, Evangelii gaudium katika maisha na utume wa Kanisa nchini Italia. Wanaendelea kukazia maisha na utume wa Wakleri sanjari na majiundo yao ya awali na endelevu, ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano kati ya Familia ya Mungu.

Ufafanuzi huu umetolewa na Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari mjini Roma, Ijumaa tarehe 30 Januari 2015. Anasema, Kongamano la kikanisa kitaifa litakalofanyika Jimbo kuu la Firenze kuanzia tarehe 9 hadi tarehe 13 Novemba 2015 litaweka dira na mkakati wa maisha na shughuli za kichungaji nchini Italia katika kipindi cha miaka kumi ijayo, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa Kanisa linalowajali na kuwahudumia maskini; mafao ya wengi pamoja na ujenzi wa utamaduni wa upendo na mshikamano.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.