Katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni changamoto kwa watawa wa Mashirika
mbali mbali kuhakikisha kwamba, wanajisadaka bila ya kujibakiza katika utoaji wa huduma,
kwa kusoma alama za nyakati, ili kuweza kukabiliana na changamoto mamboleo. Watawa
wanapaswa kuwa ni mashuhuda hai wa furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa
lake, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo ni chemchemi ya furaha ya kweli katika maisha
yao na kamwe, hawawezi kupta furaha ya kweli kwa kumezwa na malimwengu au kwa kupenda
mno utajiri na mali!
Hii ni changamoto inayotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki
Canada katika maadhimisho ya Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni ambayo kimsingi pia
ni Siku ya Watawa Duniani, ambayo kwa mwaka huu inakwenda sanjari na maadhimisho ya
Mwaka wa Watawa Duniani.
Watawa wanachangamotishwa kuwa kweli ni manabii,
kwa kujitahidi kumwilisha tunu msingi za maisha ya Kiinjili katika uhalisia wa maisha
yao, ili kujenga udugu, ukarimu na upendo wa dhati. Ni wajibu wa watawa kuhakikisha
kwamba, wanadumisha umoja na mshikamano, kielelezo cha neema ya Mungu inayotenda kazi
ndani mwao.
Watawa wawe tayari kujisadaka katika mchakato wa Uinjilishaji
mpya kwa kuwaendea maskini na wote wanaoishi pembezoni mwa jamii; ili kuwahudumia
na kuwafariji: wakimbizi, wahamiaji pamoja na kuwamegea katekesi ya kina; mambo ambayo
kwanza kabisa hayana budi kupata chimbuko lake katika tafakari ya Neno la Mungu, maisha
ya Sala na Sakramenti za Kanisa; wakiwa daima tayari kutafuta na kutekeleza mapenzi
ya Mungu katika maisha na utume wao. Watawa kwa njia ya karama za mashirika yao wanaweza
kusaidia mchakato wa Uinjilishaji mpya, tayari kupambana na changamoto za Uinjilishaji,
kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu.
Baraza la Maaskofu
Katoliki Canada linawataka watawa kuangalia historia ya waanzilishi wa Mashirika ya
Kitawa na Kazi za Kitume kutoka nchini humo, kwa kuwa na ujasiri wa kufanya marekebisho
makubwa, tayari kutoka kifua mbele kuwatangazia watu Injili ya Furaha, kwa njia ya
ushuhuda wenye mvuto na mashiko. Maaskofu wanawapongeza na kuwashukuru watawa kwa
kushikamana na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii na kwamba,
huduma yao ina umuhimu wa pekee katika maisha na utume wa Kanisa nchini Canada.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.