2015-01-31 09:00:34

Mafuriko Malawi!


Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, limehitimisha mkutano wake wa mwanzo wa mwaka kwa kuchambua kwa kina na mapana athari za mafuriko yaliyosababisha maafa makubwa kwa wananchi wa Malawi; utekelezaji wa maazimio ya mkutano mkuu wa kumi na nane wa AMECEA uliofanyika nchini Malawi kunako mwaka 2014; tathmini ya hija ya kitume ya Baraza la Maaskofu Katoliki mjini Vatican; hali halisi ya kisiasa na kiuchumi nchini Malawi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi limeangalia kwa uchungu mkubwa maafa yaliyosababishwa na mafuriko ambayo hayajawahi kutokea nchini humo na kusababisha watu zaidi ya elfu mbili kupoteza maisha na wilaya kumi na tano kuathirika vibaya. Maaskofu wamejiwekea mikakati ya kuratibu misaada ya dharura kwa ajili ya kuwasaidia wananchi walioathirika kutokana na mafuriko hayo ili waweze kuanza tena upya kwa imani na matumaini.

Maaskofu wamejadili pia maazimio yaliyopitishwa na Shirikisho la Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, ili kukabiliana na changamoto za Uinjilishaji unaojikita katika wongofu na ushuhuda wa imani kwa Kristo na Kanisa lake. Wameangalia kwa kina na mapana tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, changamoto na fursa zilizopo, ili kuliwezesha Kanisa kuendelea kutangaza Injili ya Familia kwa ari na moyo mkuu bila kusahau umuhimu wa ujenzi wa amani.

Maaskofu wanasema, kuna haja kwa Kanisa nchini Malawi, kuendelea kujielekeza katika Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili; kwa kuwa na mbinu mkakati wa Uinjilishaji unaowasaidia waamini kupata katekesi makini na endelevu; ili kuwajengea moyo wa toba na wongofu wa ndani; tayari kumshuhudia Kristo kwa njia ya imani tendaji katika medani mbali mbali za maisha.

Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi limetathmini hija ya kitume lililoifanya mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 12 Novemba 2014; wakaangalia pia hali ya kisiasa, kiuchumi na kijamii pamoja na kufanya tathmini ya kina kuhusu uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Malawi mwaka 2014. Baraza la Maaskofu limepitisha pia Katiba ya Chama cha Kitume cha Uamsho wa Kikatoliki pamoja na Umoja wa Wanawake Wakatoliki wa Malawi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.