2015-01-31 08:56:59

Boko Haram!


Umoja wa Afrika katika mkutano wake uliokuwa unafanyika mjini Addis Ababa, umepitisha mkakati wa kuunda kikosi maalum cha kupambana na kikundi cha Boko Haram ambacho kimekuwa ni tishio kwa amani na usalama huko Nigeria na katika nchi jirani na kwamba, hatua ya pili kwa sasa ni kuomba kibali kutoka katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Ikiwa kama mpango huu utakubaliwa, ina maana kwamba, Umoja wa Mataifa utasaidia kuchangia gharama za kupambana na kikosi cha kigaidi cha Boko Haram, huko Kaskazini mwa Afrika na kwamba, operesheni hii itaratibiwa mjini N'Djamena, nchini Chad.Tangu Cameroon, Chad na Nigeria zilipoamua kuunganisha nguvu zao dhidi ya kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, wachunguzi wa mambo wanasema, kumeanza kuonekana dalili za mafanikio.

Uamuzi wa kuunda kikosi kazi ili kupambana na Boko Haram umefikiwa katika mkutano wa baadhi ya Marais kutoka Afrika Magharibi uliokuwa unaratibiwa na Bibi Nkosazana Dlamin Zuma, Kamisheni wa Umoja wa Afrika, aliyekiri kwamba, vitendo vya kigaidi hasa vile vinavyofanywa na Boko Haram vinatishia amani, usalama, ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika. Ameitaka Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inasaidia kutoa jibu makini na lenye uhakika katika mapambano dhidi ya Boko Haram.

Umoja wa Afrika umejadili pia mbinu mkakati ya kupambana na ugonjwa wa Ebola ambao kwa kipindi cha mwaka mmoja, umesababisha maafa makubwa kwa maisha na maendeleo ya watu wengi huko Afrika Magharibi, ingawa kwa sasa maambukizi kadiri ya taarifa ya Shirika la Afya Duniani yanaendelea kupungua, lakini bado Ebola ni tishio kwa usalama na maisha ya watu wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.