2015-01-30 12:17:51

Dira ya Mkristo: kumbu kumbu hai na matumaini!


Mkristo anapokutana na Yesu kwa mara ya kwanza katika maisha yake, hana budi kutunza ndani mwake kumbu kumbu na matumaini, yanayomkirimia ujasiri wa kusongea mbele pasi na woga wala makunyanzi, tayari kushuhudia imani yake hata katika mazingira magumu.

Siku hii ni mwanzo wa kukutana na mwanga wa Kristo katika maisha, tukio ambalo linaujaza moyo wa mwamini furaha ya ajabu, kiasi hata cha kutamani kuthubutu kutenda makuu. Mwamini hana budi kuendelea kukuza na kuimarisha ujasiri, ari na ukweli; mambo yanayoibuliwa katika upendo wa kukutana na Yesu kwa mara ya kwanza katika maisha!

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, siku ya Ijumaa, tarehe 30 Januari 2015, changamoto na mwaliko kwa waamini kusonga mbele kwa ujasiri mkubwa, kwa kutambua kwamba, upendo wa Yesu unawaongoza.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, Wakristo wasiokuwa na msimamo ni hatari sana kwani ni sawa na "Mbwa anayekula matapishi yake" na kundi la pili ni wale waamini ambao kwa mara ya kwanza wanaonesha furaha kwa kuona miujiza inayotendwa na Yesu, lakini wanapokabiliwa na magumu pamoja na changamoto za kiimani, wanasinyaa na kukosa mwelekeo; hawa ndio wale ambao baada Shetani kubomolewa makazi yake katika maisha yao, anapowarudia tena, hali yao inakua mbaya zaidi, kuliko ilivyokuwa hapo mwanzo, kama anavyosimulia Yesu mwenyewe katika Maandiko Matakatifu. Waamini waoneshe ujasiri wa kushinda ubaya kwa kutambua kwamba, matumaini kwa Yesu, kamwe hayawezi kumdanganya mwamini.

Kumbu kumbu hai na matumaini anasema Baba Mtakatifu ni kanuni msingi katika kutunza wokovu ambao ni zawadi kutoka kwa Yesu, kwa waja wake, kwani mambo haya ni chemchemi ya imani, ili kuiwezesha mbegu ya haladali kuweza kuzaa matunda ajaa. Inasikitisha kuona kwamba, katika hija ya maisha, kuna Wakristo wengi ambao wamejikatia tamaa na kuanguka, kiasi cha kushindwa kuonana na Yesu tena, kwani wamepoteza ile kumbu kumbu hai na matumaini.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Mwenyezi Mungu ili aweze kuwasaidia kutunza zawadi ya wokovu waliyoipokea kwa njia ya imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.