2015-01-29 07:41:02

Unyanyasi wa kijinsia kwa njia ya mitandao


Katika kipindi cha Mwaka 2013 zaidi ya vijana 20, 000 Barani Ulaya walinyanyaswa kijinsia kwa njia ya mitandao ya kijamii ambayo kwa sasa ni maarufu sana katika maisha ya vijana wengi, kiasi kwamba, kwa kijana ambaye hashiriki kikamilifu katika mitandao ya kijamii anaonekana kuwa ni mtu aliyepitwa na wakati. RealAudioMP3

Hili ni tatizo linalokuwa na kuongezeka siku kwa siku na madhara yake ni makubwa katika maisha, malezi na makuzi ya vijana wanaoogelea katika mitandao ya kijamii!

Baraza la Kipapa la haki na amani kwa kushirikiana na wadau mbali mbali, hivi karibuni limezindua mbinu mkakati wa kupambana na nyanyaso za kijinsia kwenye mitandao, kama sehemu ya maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 25 tangu Umoja wa Mataifa ulipotoa Azimio ya Haki ya Mtoto Duniani.

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema kwamba, malezi na makuzi ni jambo ambalo linapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza kwa vijana, ili kuzuia majanga makubwa katika maadili na utu wema yanayoweza kuibuliwa kwa matumizi haramu ya mitandao ya kijamii.

Vijana wanapaswa kuelimishwa kutambua utu na heshima inayojikita katika maisha ya vijana wenzao, kwa kuwaona kuwa ni wenzi wa maisha badala ya mwelekeo wa sasa wa vijana kutaka kupimana nguvu na kutishiana maisha kwa njia ya mitandao, mambo ambayo yanasababisha madonda makubwa katika maisha ya baadhi ya vijana. Vijana wasaidiwe kukuza na kudumisha mshikamano wa umoja, udugu na upendo, kwa kutambua kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mwenyezi Mungu.

Kampeni hii, inasimamiwa na kuendeshwa na Shirikisho la Vyama vya Watoto Wakatoliki, ambalo limekwishakusanya sahihi zaidi ya elfu kumi zinazounga mkono kampeni hii, kama anavyoeleza Bwana Olivier Duval, Rais wa Shirikisho hili wakati wa uzinduzi wa kampeni hii. Anasema, kuna haja kwa jamii kulivalia njuga tatizo hili kwani ni hatari sana kwa malezi na makuzi ya vijana kwa sasa na kwa siku za usoni.

Ni tabia inayowapelekea vijana kuvunja sheria na kanuni maadili. Kumbe, kuna haja ya jamii kuwapatia vijana hawa njia mbadala zitakazowalinda ili wasitumbukie wala kuwatumbukiza vijana wenzao katika nyanyaso za kijinsia kwa njia ya mitandao ya kijamii, mambo ambayo yamewaachia vijana wengi machungu makubwa katika maisha na makuzi yao.

Mama Flaminia Giovanelli, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema, maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari ni makubwa sana, kiasi ambacho kinawataka wazazi na walezi kushikamana na vijana wao, ili kuwapatia malezi bora, kwa kuangalia utajiri unaopatikana kutoka katika matumizi ya mitandao ya kijamii na madhara yake. Mitandao ya kijamii inaweza kuwa ni mahali ambapo vijana, wazazi na walezi wanakutana, ili kukuza na kudumisha mahusiano ya kifamilia.

Lakini ukweli wa mambo unaonesha kwamba, mitandao ya kijamii imekuwa ni uwanja wa mapambano na patashika nguo kuchanika kati ya vijana na wazazi wao; ni mahali ambapo ubinafsi na uchoyo vimeshika nafasi ya kwanza. Kumbe, kuna haja ya kuwa na matumizi bora zaidi ya mitandao ya kijamii, ili kweli isaidie kukuza na kudumisha tunu bora za maisha ya kijamii kwa kuzingatia kanuni maadili na utu wema.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.