2015-01-29 09:48:06

Katekesi kwanza!


Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa Uinjilishaji mpya kwa kutambua umuhimu wa katekesi makini katika mchakato wa Uinjilishaji mpya unaojikita katika: Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha adili na Sala, hivi karibuni, limekuwa na mkutano pamoja na wajumbe kutoka katika Tume za Katekesi za Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, ili kujadili, kupembua na kuangalia jinsi ya kuwasaidia waamini wanaotafuta maana katika maisha yao!

Wajumbe kwa pamoja wamekazia umuhimu wa kuwapatia majiundo makini wakatekumeni, ili waweze kuifahamu na hatimaye, kuikumbatia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Kuna watu wengi ambao wanataka kuifahamu imani yao kwa kina na mapana, ili waweze kusimama imara, kuiungama, kuiadhimisha, kuimwilisha na kuisali, lakini wanakumbana na mazingira ambayo ni hatari katika ukuaji wa maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili.

Mawazo mepesi mepesi, tabia ya kubeza dini na watu kumezwa mno na malimwengu ni kati ya mambo ambayo kwa sasa yanaoneka kana kwamba, ndio mfumo wa maisha ya wananchi wa Ulaya, hali ambayo inajionesha pia katika utepetevu wa imani miongoni mwa Wakristo Barani Ulaya, anasema Askofu mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa Uinjilishaji Mpya.

Anasema, kuna haja kwa Mama Kanisa kuimarisha uelewa wa Mafundisho Tanzu ya Kanisa; mikakati na shughuli za kichungaji zinazotekelezwa na Kanisa mahalia sanjari na ukuaji wa Mkristo mmoja mmoja katika maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili mintarafu katekesi ya kina. Ikumbukwe kwamba, katekesi ni muhtasari wa mafundisho ya Kanisa yanayojikita katika kanuni ya Imani, maisha ya Kisakramenti, Amri kumi za Mungu na Sala za Kanisa; hii ndiyo mihimili mikuu inayodhihirisha na kushuhudia imani na maisha ya Kanisa.

Mchakato wa Uinjilishaji mpya unapania kukuza na kudumisha ari na moyo wa shughuli na mikakati ya kimissionari; mambo ambayo Baba Mtakatifu Francisko anasema yanamwilishwa katika Katekesi, inayomwezesha mwamini kutolea ushuhuda imani yake kwa Kristo na Kanisa lake, tayari kujikita katika toba na wongofu wa ndani, ili kukumbatia maisha mapya.

Uinjilishaji mpya unalihamasisha Kanisa kutoka kifua mbele, ili kuwashirikisha Watu wa Mataifa, utajiri unaofumbatwa katika maisha na utume wake, ili kuwawezesha watu kukutana na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, tayari kuonja huruma na upendo wake usiokuwa na kifani. Mkutano huu umewashirikisha Maaskofu wakuu wa Idara na Tume za Katekesi kutoka katika Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, CCEE.

Taarifa za wajumbe zinaonesha jinsi ambavyo Makanisa mahalia yanavyotoa kipaumbele cha pekee kwa ajili ya katekesi sanjari na kuhakikisha kwamba, Makatekista wanafundwa vyema, ili waweze kutekeleza dhamana na utume wao barabara.

Ikumbukwe kwamba, Makatekista ni kundi muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa, hawa ndio wanaofundisha imani, wanaowaandaa watoto, vijana na wakatekumeni kupokea Sakramenti za Kanisa. Ni watu wanaojisadaka kwa ajili ya kufundisha dini shuleni na parokiani, wakiheshimiwa na kuthaminiwa, watachangia kwa kina na mapana katika katekesi, maisha na utume wa Kanisa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.