2015-01-29 09:06:49

Athari za mafuriko Malawi


Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa FAO, linaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuchangia kwa hali na mali ili kuikwamua Malawi, ambayo kwa siku za hivi karibuni imekumbwa na mafuriko makubwa ambayo yamesababisha maafa na uharibifu mkubwa wa miundo mbinu, mambo ambayo yanahatarisha uhakika wa usalama wa chakula nchini Malawi.

Taarifa zinaonesha kwamba, zaidi ya watu 170, 000 wamelazimika kuyahama makazi yao kutokana na mafuriko, bado kuna watu 153 kutoka Wilaya ya Nsanje, hawajulikani mahali walipo. Inasemekana kwamba, zaidi ya watu 116, 000 wamepoteza mazao na mifugo yao. Sehemu kubwa ya ardhi imemezwa na mafuriko, kiasi kwamba, Serikali imetangaza hali ya hatari kwa Wilaya 15 kati ya 28. Wilaya za Chikwawa, Nsanje na Phalombe zimeathirika vibaya sana.

Serikali ya Malawi inakadiria kwamba, kunahitajika walau kiasi cha dolla za kimarekani millioni 16 ili kusaidia kuokoa sekta ya kilimo na mifugo nchini humo. Kama Malawi haitapatiwa msaada haraka iwezekanavyo, kuna hatari kwamba, itakumbukwa na baa la njaa kwa siku za usoni, kwa kutambua kwamba, asilimia 86% ya wananchi wa Malawi wanategemea maisha yao kutoka katika sekta ya kilimo.







All the contents on this site are copyrighted ©.