2015-01-29 08:53:58

Al-Shabaab kuendelea kumegeka?


Kitendo cha Zakariya Ismail Hersi, aliyekuwa kiongozi mkuu wa inteligensia ya Kikundi cha kigaidi cha Al-Shabaab, ambacho kwa miaka ya hivi karibuni kimeitikisa Somalia na nchi jirani kutokana na mashambulizi ya kigaidi, kuamua kubwaga manyanga na kuacha kujihusisha tena na matumizi ya nguvu na badala yake, kuwataka, wanajeshi wa Al-Shabaab, kuanza mchakato wa upatanisho, ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kimepokelewa kwa matumaini makubwa.

Wachunguzi wa mambo wanasema, kifo cha Godane aliyekuwa ni kiongozi mkuu wa Al-Shabaab, mwezi Septemba, 2014 kimeacha pengo kubwa, kwani kiongozi huyu alikuwa anatawala kwa mkono wa chuma, hali ambayo imepelekea mgawanyiko ndani ya Kikundi cha Al-Shabaab.

Serikali ya Somalia kwa kusaidiwa na Vikosi vya ulinzi na usalama kutoka Umoja wa Afrika inaendelea kutawala sehemu kubwa ya Somalia, licha ya mashambulizi ya mara kwa mara yanayofanywa na kikundi cha Al-Shabaab. Wapenda amani, sehemu mbali mbali za dunia wamezipokea habari hizi kwa matumaini makubwa!







All the contents on this site are copyrighted ©.