2015-01-28 07:24:57

Soweto kumechafuka!


Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini, linalaani matukio ya uvunjifu wa amani na utulivu yaliyojitokeza huko Soweto, Afrika ya Kusini, kwa maduka ya wageni kuvunjwa na watu kuwapora mali. Katika matukio haya kuna baadhi ya watu ambao wamepoteza maisha na wengine wengi kujeruhiwa. Jeshi la Polisi linawashikilia watu zaidi ya 120 kuhusiana na matukio haya na kwamba, kuna idadi kubwa ya wafanyabiashara waliokutwa na silha kinyume cha sheria.

Uvunjifu wa amani na utulivu ulijitokeza hivi karibuni pale ambapo kijana mmoja alipigwa risasi na kuuwawa na mfanyabiashara mmoja huko Soweto katika tukio la kujaribu kupora. Maaskofu wanawataka wananchi kuzingatia utawala wa haki na sheria na kamwe wasijichukulie sheria mikononi mwao, kwani wanaweza kusababisha madhara makubwa kwa watu na mali zao. Vitendo vya kuvunja majengo na miundo mbinu vinachangia hata kuharibu maadili na utu wema; mambo yanayolichafua taifa.

Maaskofu wanasikitika kusema kwamba, katika matukio haya kuna watu ambao wamepoteza maisha yao; wanasali na kuwaombea wale wote waliofikwa na majanga haya na wanapenda kuonesha mshikamano wao wa dhati na wafanyabiashara ambao wameshuhudia maduka na biashara zao zikiharibiwa na watu waliokuwa na hasira. Matukio yote haya yanaendelea kusababisha machungu katika maisha ya watu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini, linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuwasaidia wale ambao wameathirika kutokana na matukio ya uvunjifu wa amani na utulivu huko Afrika ya Kusini. Wananchi watoe ushirikiano wa dhati, ili wahusika waweze kufikishwa kwenye mkondo wa sheria. Wazazi na walezi watambue dhamana na wajibu wa kuwalea watoto wao kwa kuzingatia kanuni maadili na utu wema.







All the contents on this site are copyrighted ©.