2015-01-28 07:40:01

Msitumie nguvu ya fedha kukumbatia utamaduni wa kifo!


Kardinali Seàn O'Malley, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Boston, Marekani, amepongeza uamuzi wa Serikali ya Marekani kutokutoa fedha ya walipa kodi kwa ajili ya kugharimia vitendo vya utoaji mimba na kwamba, hii ni hatua muhimu sana katika mchakato wa kulinda watoto ambao bado hawajazaliwa, jambo linaoonesha utashi wa wananchi wengi wa Marekani.

Sheria ya kufuta ruzuku ya serikali kwa ajili ya kugharimia vitendo vya utoaji mimba, ilipitishwa tarehe 22 Januari 2015, wakati wa maandamano makubwa kupinga sheria ya utoaji mimba nchini Marekani. Serikali kwa sasa inakazia umuhimu wa ukweli na uwazi katika matumizi ya fedha za umma. Kardinali O'Malley anasema, umefika wakati kwa Serikali kuheshimu maamuzi na sheria zake ambazo zimekuwepo nchini humo kwa takribani miaka thelathini na saba na kwamba, isitumie nguvu ya fedha kuhamasisha vitendo vya utoaji mimba na wala isiwalazimishe walipa kodi kuchangia mauaji.

Serikali ina wajibu wa kuwasaidia watu kupokea zawadi ya maisha badala ya kuwahamasisha kutoa mimba. Umefika wakati kwa wananchi wa Marekani kuchagua sera za bima ya afya zinazoendana na kanuni maadili na utu wema.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.