Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano tarehe 28 Januari 2015 ameendelea na Katekesi yake
kuhusu Familia, kwa kuangalia: utu, dhamana na nafasi ya Baba wa familia, jina ambalo
Wakristo wamefundishwa na Yesu mwenyewe kumwita Mwenyezi Mungu; jina lenye utajiri
mkubwa wa mahusiano katika jamii.
Jambo la kusikitisha anasema Baba Mtakatifu
katika jamii mamboleo, kuna mgogoro wa dhana ya uelewa wa Ubaba ambao kwa wengi unaonekana
kuwa ni mtu mwenye madaraka na hata wakati mwingine ni mtu mkatili; mambo yanayochanganya
kuhusu uelewa na dhamana ya Baba ndani ya familia.
Baba Mtakatifu anasema,
leo hii inawezekana kuzungumzia kuhusu "kutokuwepo" kwa Baba kama kielelezo katika
jamii, lakini ikumbukwe kwamba, dhamana na nafasi ya Baba ni muhimu sana katika familia,
kwani wao ni mfano na mwongozo kwa watoto katika hekima na fadhila. Bila ya uwepo
wa Baba, watoto wengi wanajisikia kuwa "yatima", wakiachwa huku wanatangatanga na
hivyo kukosa mwelekeo wa makuzi pamoja na maendeleo yao.
Baba Mtakatifu anasema,
hata jamii ina wajibu wa kuhakikisha kwamba, inawalinda na kuwatunza watoto, ili wasibaki
na kujisikia kuwa ni yatima, bila mawazo, tunu msingi za maisha, matumaini na fursa
za kazi na ukweli mtimilifu katika maisha ya kiroho. Yesu aliwaambia wafuasi wake
kwamba, kamwe hatawaacha yatima. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuimarisha na kupyaisha
tena utambuzi wa ubaba na hivyo kuanza mchakato wa kupata mababa wema kwa ajili ya
mafao na ustawi wa familia, Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake.
Baba Mtakatifu
Francisko akizungumza na waamini pamoja na mahujaji kwa lugha mbali mbali amewataka
kumsikiliza kwa makini Yesu anayewafunulia Mwenyezi Mungu kama Baba anayewapenda na
kuwaunda wote ili waweze kuwa ndugu wamoja. Waamini waendelee kujifunza kutoka kwa
watakatifu ili kuishi kwa nguvu ya sala, huku wakijitahidi kushughulikia wokovu wa
ndugu zao. Roho Mtakatifu awasaidie ili waweze kuwa kweli ni watakatifu.
Baba
Mtakatifu amezikumbuka na kuziombea familia mbali mbali zinazoogelea katika shida
na magumu ya maisha, zitambue kwamba, wao ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa
ajili ya Jumuiya za Kikristo. Ukosefu wa upendo, dhana na uelewa wa Baba ndani ya
familia unaweza kugumisha mchakato wa kujenga mahusiano na Mwenyezi Mungu ambaye ni
Baba.
Waamini wanaalikwa kusali kwa ajili ya baba katika familia, ili waweze
kutekeleza dhamana na wajibu wao kikamilifu pamoja na kuendelea kuwa ni alama ya upendo
kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Mwishoni, Baba Mtakatifu anawataka waamini na mahujaji
wanaotembelea kwenye Makaburi ya Watakatifu Petro na Paulo, wapate mwamko na ari mpya
ya kutaka kushuhudia Ukristo wao katika familia na jamii kwa ujumla wake.
Katika
kumbu kumbu ya Mtakatifu Thoma wa Akwino, Padre na Mwalimu wa Kanisa, Baba Mtakatifu
anawataka vijana kujielekeza zaidi katika masomo, ili kunoa akili na utashi wao kwa
ajili ya huduma ya Injili. Imani ya Mtakatifu Thoma, iwasaidie wagonjwa kumkimbilia
Yesu hata katika nyakati za majaribu; upole wake uwe ni kielelezo cha mahusiano mema
kati ya wanandoa ndani ya familia.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.