2015-01-27 07:37:24

Umoja na mshikamano wa kitaifa!


Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, limehitimisha mkutano wake wa mwanzo wa mwaka, kwa kuwataka waamini na wananchi wote, kujikita katika ujenzi wa msingi wa haki, amani, upatanisho na umoja wa kitaifa baada yao nchi kwa miaka kadhaa kuogelea katika dimbwi la machafuko na vita; mambo ambayo yamepelekea maafa makubwa kwa watu na mali zao. RealAudioMP3

Wananchi wanataka kujikita katika mchakato wa haki, amani, msamaha na upatanisho wa kitaifa, kama chachu ya kuwaletea maendeleo endelevu. Hii ni changamoto ya kuondokana na mawazo ya kuweza kupata mafanikio katika maisha kwa kukumbatia ushirikina, ambao pia umekuwa ni chanzo cha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia pamoja na uvunjifu wa mustakabali wa taifa. Wananchi watakakiwa kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yao kwa kukataa kishawishi cha ulevi wa kupindukia, rushwa, ufisadi pamoja na kukumbatia utamaduni wa kifo.

Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, linawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kujifungwa kibwebwe ili kuganga magonjwa ya kiroho, kimwili na ukosefu wa maadili na utu wema. Maaskofu wanataka wananchi kutekeleza wajibu wao kikamilifu na wote kwa pamoja, washikamane ili kupambana kufa na kupona na majanga ambayo yanaendelea kukwamisha mchakato wa maendeleo ya watu: kiroho, kimwili na kimaadili. Serikali inawajibika kupambana pia na rushwa pamoja na ufisadi, kwa kuhakikisha kwamba, utawala wa sheria unajengeka na kudumishwa miongoni mwa wananchi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, linawataka wananchi kujenga na kudumisha haki, amani na utulivu, hasa wakati huu wanapojiandaa kwa ajili ya uchaguzi mkuu. Wananchi wajikite katika ukomavu wa maisha ya kiroho na kimaadili, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa tunu msingi zinazowaunganisha wananchi wote wa Pwani ya Pembe. Wananchi wanaonywa tabia ya kuuza ardhi kuwa ni hatari kwa maendeleo yao ya siku za usoni.

Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, mwishoni, linawataka vijana kujikita katika tunu msingi za kimaadili na utu wema na kukataa katu katu kutumiwa na baadhi ya wanasiasa uchwara kwa ajili ya mafao yao binafsi. Vijana wajenge moyo na tabi ya kufanya kazi halali na kwamba, hakuna sababu ya kukata tamaa kwani Pwani ya Pembe ni nchi ya matumaini, wakitaka wanaweza kupata maisha bora zaidi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.