2015-01-27 08:25:22

Msikate tamaa!


Wakristo wengi mjini Niamey, nchiniNiger, Jumapili iliyopita wameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na Liturujia ya Neno pasi na nguo wala vyombo vya ibada, baada ya Makanisa kadhaa kuchomwa moto hivi karibuni kutoka na kinzani za kidini. Viongozi wa Kanisa wanaendelea kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutokata tamaa, bali waendelee kujikita katika majadiliano ya kidini, ili amani, upendo na mshikamano viweze kutawala tena katika mioyo ya watu kwa kuondokana na chuki pamoja na kinzani za kidini, ambazo kwa sasa hazina mvuto wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya watu!

Viongozi wa Kanisa wanasema, uharibifu uliofanywa kwenye Parokia za Jimbo kuu la Niamey, nchini Niger ni zaidi ya millioni mbili za Euro. Ili kuonesha umoja na mshikamano wa Kikanisa, waamini wa Jimbo kuu la Niamey wameamua kuchangia sehemu ya mshahara wao, ili kusaidia mchakato wa ujenzi wa Parokia na nyumba za Ibada zilizochomwa moto hivi karibuni kutokana na msimamo mkali wa kidini. Sehemu ya pili ya mchakato huu ni kuendeleza majadiliano ya kidini, ili kujenga na kudumisha umoja, upendo na mshikamano wa kidugu.

Viongozi wakuu wa Kanisa wameamua kutembelea Parokia zote Jimboni humo, ili kuwaimarisha waamini katika msingi wa haki, amani, msamaha na upatanisho. Wakleri na waamini wanaendelea kusali kwa ajili ya amani na utulivu, huku wakimwomba, Bikira Maria awaombee, ili kweli waendelee kuwa ni watu wenye matumaini, upendo, msamaha na upatanisho. Licha ya magumu na changamoto wanazokabiliana nazo, waamini na watambue kwamba, bado wanahamasishwa kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.