2015-01-27 10:57:47

Mapenzi ya Mungu!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumanne, tarehe 27 Januari 2015 amekumbusha kwamba, ukosefu wa utii na kushindwa kutekeleza mapenzi ya Mungu, kulimpelekea mwanadamu kukosa Paradiso na kwamba, utii wa Adamu ulimfungulia njia ya mbinguni. Yesu Kristo anawafundisha wafuasi wake kujikita katika utii, kwa kutekeleza mapenzi yake hapa duniani, tayari pia kushiriki katika utukufu wake mbinguni.

Yesu katika maisha na utume wake alionesha utii mkubwa kwa Baba yake wa mbinguni, lakini bila kusahau kwamba, Bikira Maria ni mama aliyeonesha utii wa hali ya juu kwa Malaika Gabrieli, alipokubali mpango wa Mungu katika maisha yake. Na kwa kukubali kwake, Bikira Maria akaanzisha safari ya mshikamano na binadamu.

Baba Mtakatifu anasema, anaendelea kusali ili Mwenyezi Mungu aweze kumkirimia ujasiri wa kufanya mapenzi yake, lakini zaidi kuyafahamu mapenzi haya katika maisha na katika maamuzi ambayo anapaswa kuyafanya kwa wakati huu; namna ya kuratibu mambo mbali mbali. Kimsingi, sala kwa ajili ya kufanya mapenzi ya Mungu ni sala inayotaka kufahamu mapenzi hayo ya Mungu na kuyamwilisha katika uhalisia wa maisha. Ni dhamana nyeti anasema Baba Mtakatifu.

Si rahisi kuyafahamu mapenzi ya Mungu, kumbe, waamini wanapaswa kumwomba Mwenyezi Mungu, awakirimia neema ya kutambua mapenzi yake na kuyatekeleza kama alivyofanya Yesu alipouambia umati mkubwa wa watu uliokuwa unamsikiliza, mama na ndugu zake ni wale wote wanaotekeleza mapenzi ya Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.