2015-01-27 07:58:56

Familia ni shule ya kwanza ya upendo!


Baraza la Maaskofu Katoliki Poland, linaadhimisha Mwaka wa Upendo, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, ili wao pia waweze kuonja upendo na neema inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. RealAudioMP3

Familia ya Mungu nchini Poland inaadhimisha tukio hili, miaka arobaini baada ya utawala wa Kikumonusti kufutilia mbali kitengo cha misaada cha Kanisa Katoliki, Caritas nchini humo, kilichoanzishwa baadaye kunako mwaka 1990.

Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas ni kati ya vitendo ambavyo vinafanya utume wake kwa ufanisi mkubwa katika Majimbo na Parokia mbali mbali nchini Poland, hasa kwa ajili ya kuwasaidia na kuwahudumia maskini na watu wanaopatwa majanga katika maisha. Ni kitendo ambacho kimeliwezesha Kanisa kukesha na wagonjwa, wazee, watoto yatima na watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi. Caritas imezijengea uwezo familia mbali mbali nchini Poland, ili ziweze kutekeleza dhamana na wajibu wake wa kulea na kutunza watoto kadiri ya mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Mwezi Desemba, 2014, aliwakumbuka waamini nchini Poland kwa kuadhimisha Mwaka wa Upendo, kwa kuonesha mshikamano na maskini pamoja na wote wanaosukumbizwa pembezoni mwa jamii. Caritas katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwake tena nchini Poland, imeendelea kuwasaidia watoto wengi wanaoishi katika mazingira hatarishi na magumu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Poland linabainisha kwamba, kipaumbele cha kwanza katika maadhimisho ya Mwaka wa Upendo ni familia, ili kuziwezesha familia kujenga na kuimarisha tunu msingi za maisha, ili hatimaye, kuziwezesha familia nchini humo kuwa kweli ni kitalu na shule ya kwanza ya upendo na mshikamano kati ya watu!







All the contents on this site are copyrighted ©.