Boko Haram inaua hata chembe cha majadiliano ya kidini!
Askofu mkuu Ignatius Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria anasema,
wakati huu Nigeria inapojiandaa kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika
mwezi Februari, 2015, Kikundi cha Boko Haram kinaendelea kuzidisha mashambulizi ya
kushtukiza na hivyo kusababisha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.
Kuna hatari
kwamba, Boko Haram ikatawala eneo lote la Kaskazini Mashariki mwa Nigeria na kwamba,
lengo lao ni kuhakikisha kuwa wanatala mji wa Maiduguri. Ikiwa kama lengo hili litafanikiwa,
miji mingine iliyoko kando kando ya Maiduguri itaanguka kwa urahisi sana.
Askofu
mkuu Kaigama katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema, si rahisi kuweza kufanya
majadiliano ya kidini na Kikundi cha Boko Haram kwani hawa ni magaidi wanaoendelea
kusababisha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia na hivyo kupandikiza mbegu ya chuki
na uhasama kati ya Wakristo na Waislam. Na kwa maneno mengine, Boko Haram inaendelea
kuvuruga mchakato wa majadiliano ya kidini nchini Nigeria.
Ni matumaini ya
Maaskofu wa Nigeria kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itaguswa na mahangaiko pamoja na
mateso ya wananchi wa Nigeria na hivyo wataweza kuwaunga mkono katika mchakato wa
kupambana na Boko Haram. Hii inatokana na ukweli kwamba, Serikali ya Nigeria imeonesha
udhaifu mkubwa dhidi ya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram.
Baraza la Maaskofu
Katoliki Nigeria linasema kwamba, uchaguzi mkuuu na atakayeingia madarakani si kipaumbele
chao kwa sasa, Kanisa linapenda kuona viongozi watakaochaguliwa na wananchi kwa mwaka
huu, wanakuwa kweli ni watu wanaotafuta mafao ya wengi, haki, amani, utulivu na maendeleo
ya wananchi wa Nigeria. Inasikitisha kuona kwamba, ukosefu wa haki, amani na utulivu
ni matunda ya rushwa na ufisadi.
Kwa bahati mbaya, viongozi wengi wa kisiasa
nchini Nigeria wanatafuta mafao yao binafsi, ndiyo maana haya hawajishughulishi kikamilifu
kutafuta haki, amani na utulivu na badala yake wanaendelea kujikita katika kampeni,
ili wapate ridhaa ya kuongoza Nigeria. Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki
Nigeria kwamba, uchaguzi mkuu wa mwaka huu, utaweza kuwaamsha wananchi wa Nigeria
kuchagua hatima ya maisha yao kwa siku za usoni, kwa kufanya maamuzi machungu, ili
kuwapatia ridhaa viongozi watakaowaletea maendeleo ya kweli!
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.