Baba Mtakatifu Francisko amewaandikia barua Makardinali wateule ishirini, watakaosimikwa
rasmi hapo tarehe 14 Februari 2015, kwa kuwakumbusha kwamba, ukardinali ni wito katika
huduma kwa Familia ya Mungu na wala si kilele cha taaluma wala kielelezo cha madaraka
na ukuu. Baba Mtakatifu anawaalika Makardinali wateule, kuendelea kuonesha unyenyekevu
unaojikita katika huduma makini kwa Familia ya Mungu.
Kwa namna ya pekee,
Baba Mtakatifu anawaalika Makardinali wateule kusherehea dhamana hii kwa kuwa na kiasi
na kamwe wasimezwe na malimwengu na hivyo kuwaondoa kutoka katika mwelekeo sahihi
wa Fumbo la Msalaba wa Kristo. Kwa kuteuliwa kuwa Kardinali kunamaanisha kwamba, wao
sasa ni sehemu ya Jimbo kuu la Roma, ambamo wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa
Mashuhuda amini wa Ufufuko wa Kristo, tayari kujisadaka wao wenyewe hadi tone la mwisho
la damu yao, kama ikibidi.
Baba Mtakatifu anawaalika Makardinali wateule kujiandaa
kupokea dhamana hii kwa sala na kufunga. Anawatakia amani na furaha na mwishoni, anawaalika
kuendelea kumsindikiza katika maisha na utume wake kwa njia ya sala.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.