2015-01-23 11:50:51

Walei wana mchango mkubwa katika ujenzi wa familia!


Baraza la Kipapa la Familia kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Sinodi ya Maaskofu kuanzia tarehe 22 Januari hadi tarehe 24 Januari 2015 wameandaa kongamano la kimataifa, linalovishirikisha vyama 80 ya kitume kutoka sehemu mbali mbali mbali za dunia, ili kutoa mchango wao katika mchakato wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayofanyika mwezi Oktoba, 2015 hapa mjini Vatican.

Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la familia anasema kwamba, vyama vya kitume vinamchango mkubwa katika kukuza na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Tema ya familia ni nyeti na muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa ndiyo maana, matukio ya kifamilia yanafuatiliwa kwa udi na uvumba na vyombo vya upashanaji habari.

Ulimwengu mamboleo umegubikwa sana na ubinafsi na uchoyo; mambo yanayochangia mipasuko na kinzani za kijamii; ubaguzi na utenganio Kanisa halina budi kuwasaidia waamini kuwa kweli ni mashuhuda wa Injili ya Familia, kwa maneno na matendo yao mema; yenye mvuto na mashiko kwa jirani zao. Utamaduni mamboleo kwa bahati mbaya, umeendelea kubeza tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kiasi cha kukosa mvuto kutoka kwa vijana wa kizazi kipya, wanaopenda kuendelea kubaki nyumbani kwa wazazi wao na mbaya zaidi pasi na kufunga ndoa, huku wakiendeleza uchumba sugu!

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican anasema, Askofu mkuu Vincenzo Paglia, wamewachangamotisha sana waamini walei, kusimama kidete, kulinda, kutetea, kudumisha na kutangaza Injili ya Familia. Familia inawajibu wa kusimama na kujitetea yenyewe dhidi ya mashambulizi kutokana na utamaduni wa kifo na sera zinazosigana na mpango wa Mungu. Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu yanapania kuwajengea waamini uwezo wa kutangaza Injili ya Familia kati ya Watu wa Mataifa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.