2015-01-23 09:25:16

Uponywaji wa kimwili na Yesu ni ishara ya uponyaji mwingine muhimu zaidi... Papa


Alhamisi Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Ibada ya Misa katika Kanisa dogo la Mtakatifu Marta, homilia yake ililenga zaidi juu ya Injili ya siku (Marko 3: 7-12), ambayo inaelezea jinsi makundi ya watu walivyokusanyika kutoka pande zote kwa lengo la kuja kukutana na Yesu. Papa anasema watu wa Mungu waliona katika Bwana, kuna "tumaini". Tumaini waliloliona katika njia zake za utendaji na mafundisho yenye kugusa moyo , kwa sababu yalikuwa na nguvu ya Neno la Mungu.

Papa aliendelea kueleza kwamba , watu walikuwa wamechoka na njia za ufundishaji wa walimu wa Sheria wa wakati huo, ambao walibebesha zaidi mzigo mzito mabega mwa watu kwa amri nyingi, maagizo mengi, ufundishaji amba o haukugusa mioyo ya watu. Lakini ufundishaji uliofanywa na Yesu uligusa mioyo ya watu , kama ilivyokuwa hotuba yake mlimani juu ya Heri. Na hivyo watu walichochewa na Roho Mtakatifu kwenda kumwona Yesu.


Papa ameasa hata kwa nyakati hizi , Yesu bado yupo kati yetu. Lakini tunahitaji kuwa na nia safi katika kumtafuta Yesu , si kwenda kumtafuta kwa nia ya uponyaji wa maradhi ya kimwili tu, lakini nia hiyo ya kwenda kumtafuta ni lazima iwe safi tangu mwanzo wake , kumtafuta kwa bidii kwa ajili ya uponywaji wa kiroho. Bahati mbaya sisi binadamu hatufanyi bidii hiyo ya kumtafuta kwa manufaa ya kiroho , wala hatuna muda na Mungu. Lakini katika hija ya kujitakasa, inatuhitaji kutenga muda wa kuwa na Mungu. Papa alieleza akitazamisha kwa jinsi watu wengi huenda kumtafuta Mungu katika madhabahu mbalimbali , lakini wengi wao, ni kwa ajili ya uponyaji wa mambo ya kimwili , hujitupa miguuni mwake na kumgusa , ili uwezo wake uwaponye, lakini si uponywaji wa Roho. .

Papa anasema, ziara za hija tunazofanya na isiwe kwa sababu Yesu kuponywa mwili au matatizo. Unapaswa kutambua kuwa uponywaji wa mwili ni ishara ya uponyaji mwingine, muhimu zaidi kuponywa kiroho, kama ilivyoandikwa katika waraka kwa Waebrania (7:25), "Yesu ni daima ana uwezo wa kuwaokoa wale wanao mkaribia Mungu katika njia yake, maana yeye anaishi milele akiwaombea kwa Mungu.


Papa aliendelea kusema, ni muhimu leo hii, kutambua kwamba, Yesu amesimama mbele ya Baba, akitolea sadaka maisha yake, kwa ajili ya wokovu wetu, anaonyesha majeraha yake kwa Baba kama malipo ya wokovu wetu. Hivyo ndivyo ilivyo kila siku, Yesu anaingilia kati katika maisha yetu , hutuombea. Nasi tunapaswa kila siku, na hasa wakati tunapoanguka katika majaribu, kwa jambo moja au jingine, tukumbuke kwamba, yupo anayetuombea msamaha kwa Mungu, anatuombea daima.

Papa ameonya kwamba kwa mara nyingi binadamu husahau kwamba Yesu alikwenda Mbinguni, na kumtuma Roho Mtakatifu. Hii si simulizi kama hadithi lakini ni ukweli halisi. Hata sasa, katika kila wakati, Yesu hutuombea. Kila tunaposali sala hii: 'Bwana Yesu, nihurumie mimi mdhambi, Yeye hulichukua ombi hili kwa Baba kwa ajili yetu.

Papa alieleza na kuhitimisha kwa kuomba ili maisha yetu ya Kikristo, yaweze kuwa na imani zaidi kwamba tumeokolewa naye Yesu Kristo ambaye kwa wakati huu ameketi upande wa kulia wa Baba, akituombea. Na akaomba kwa Bwana , Roho Mtakatifu atuwezeshe kuelewa mambo haya.








All the contents on this site are copyrighted ©.