2015-01-23 09:48:21

SPLM Sudan ya Kusini ni kicheko tupu Arusha!


Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amewapongeza wadau mbali mbali kutoka Barani Afrika waliosaidia kukamilisha mchakato wa kuwaunganisha tena viongozi wakuu wa Chama cha Ukombozi cha SPLM cha Sudan ya Kusini, kilichokuwa kimemeguka kutokana na machafuko ya kisiasa kati ya Rais Salva Mayardit Kiir wa Sudan na Makamu wake Bwana Riek Machar; tukio ambalo limetiwa sahihi mjini Arusha, tarehe 21 Januari 2015 na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa viongozi kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Afrika.

Rais Kikwete anasema, hii ni siku inayofungua ukurasa mpya wa matumaini ya amani na upatanisho wa kitaifa na hivyo kusahau machafuko ya kisiasa yaliyoitumbukiza Sudan ya Kusini katika vita ya wenyewe kwa wenyewe, kiasi cha kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Ukweli, uwazi, uvumilivu, mafao ya wengi na umoja wa kitaifa, ni mambo msingi ambayo yamewezesha tena juhudi za majadiliano ya kina kuzaa matunda yanayokusudiwa. Hiki sasa ni kipindi upatanisho, uponyaji na ujenzi wa Chama cha Ukombozi cha SPLM, ili amani iweze kutawala tena na watu kujikita katika mchakato wa kujiletea maendeleo yao wenyewe, changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, mkataba huu unaimarishwa na kudumishwa.

Rais Kikwete amewakumbusha viongozi hawa kwamba, kwa mara ya kwanza haitakuwa vigumu, lakini waendelee kujenga utamaduni wa majadiliano na kutafuta suluhu ya matatizo na changamoto watakazokutana nazo kwa amani na utulivu na kwamba, kuna nchi za Kiafrika ambazo ziko tayari kusaidia mchakato wa amani, upatanisho na maendeleo Sudan ya Kusini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.