2015-01-22 09:07:10

Lindeni Injili ya uhai!


Baba Mtakatifu Francisko anawatia ari na moyo mkuu waandaaji wa maandamano ya kutetea Injili ya Uhai yanayotarajiwa kufanyika mjini Paris, Ufaransa, Jumapili ijayo tarehe 25 Januari 2015. Askofu mkuu Luigi Ventura, Balozi wa Vatican nchini Ufaransa anasema kwamba, Baba Mtakatifu anawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao.

Wakati huo huo, Baraza la Kipapa kwa ajili ya familia linabainisha kwamba, maisha ya binadamu ni matakatifu, kumbe yanapaswa kuthaminiwa, kulindwa na kuendelezwa. Kutokana na changamoto zinazoendelea kujitokeza dhidi ya tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, Baba Mtakatifu Francisko anawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushiriki kikamilifu pasi na kuchoka wala kukata tamaa katika mchakato wa ujenzi wa utamaduni wa upendo na Injili ya Uhai.

Maandamano haya ambayo yatafanyika siku ya Jumapili mchana ni kielelezo cha Familia ya Mungu nchini Ufaransa kupinga utamaduni wa kifo unaofumbatwa katika sheria za utoaji mimba; ili kuheshimu na kutangaza Injili ya uhai inayojikita katika utamaduni wa upendo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.