Kardinali Oswald Gracias, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani
Asia anasema, hija ya kitume ya Baba Mtakatifu nchini Ufilippini, imewakirimia wananchi
matumaini mapya na furaha, baada ya kukabiliana na majanga, yaliyosababisha uchungu
na majonzi mengi. Uwepo wa Baba Mtakatifu nchini Ufilippini, limekuwa ni tukio la
furaha kuu, ambalo limewasaidia waamini kutambua tena umuhimu wa wao kujikita katika
tunu msingi za maisha ya Kiinjili.
Itakumbukwa kwamba, Kardinali Gracias ni
kati ya wale Makardinali wanane walioteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko, ili kumpatia
ushauri wa kina katika mchakato wa mageuzi katika Sekretarieti ya Vatican kama yalivyoamriwa
na vikao vya Makardinali. Anasema, Baba Mtakatifu Francisko anapenda kutoa kipaumbele
cha pekee kwa Bara la Asia, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya unaojikita
katika majadiliano ya kidini na kitamaduni, ili Injili ya Kristo isaidie kujenga na
kuimarisha misingi ya haki, amani na maridhiano kati ya watu.
Baba Mtakatifu
Francisko nchini Ufilippini amewaonjesha upendo na wao wakajibu kwa upendo pasi na
unafiki, kiasi cha kuwashangaza walimwengu, watu millioni saba, walipojitokeza mjini
Manila kwa ajili ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na Papa Francisko, siku ya
mwisho ya hija yake ya kitume mjini Manila. Ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa Familia ya
Mungu nchini Ufilippini, umegusa undani wa maisha yao na kwamba, Injili ya Kristo
ni msingi thabiti wa maisha, changamoto ya kuhakikisha kwamba, imani inamwilishwa
katika matendo kwa njia ya ushuhuda wenye mvuto na mashiko kwa watu.
Kwa upande
wake Kardinali Orlando Quevedo kutoka Ufilippini anasema, changamoto ya kiimani iliyotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko kwa Familia ya Mungu nchini Ufilippini, itakuwa ni chachu
ya kukoleza imani katika matendo, hasa wakati huu wananchi wengi wa Ufilippini wanapojitahidi
kunyanyuka tena kutoka katika janga la Yolanda, lililowagusa na kuwatikisa hata katika
imani yao.
Baba Mtakatifu amependa kuonesha upendo na mshikamano kwa maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, ndiyo maana, kulikuwa na ujumbe mkubwa
wa wahanga wa dhoruba ya Yolanda,ambao walikutana wakazungumza na hatimaye, kupata
chakula cha mchana na Baba Mtakatifu Francisko, tukio ambalo limeacha chapa ya kudumu
katika mioyo ya maskini wengi. Hiki ni kielelezo cha mshikamano wa upendo kati ya
Kanisa la Kiulimwengu na Kanisa mahalia.
Uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko
nchini Ufilippini, umekuwa ni ushuhuda wenye mvuto na mashiko makubwa; wameonja upendo
na huruma yake; wakaguswa na unyenyekevu na upendo unaobubujika kutoka katika undani
wa maisha. Ameishukuru na kuipongeza Serikali ya Ufilippini kwa kuanzisha mchakato
wa haki, amani na upatanisho Kusini mwa nchi hiyo, kwa kuheshimu pia uhuru wa kuabudu.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.