2015-01-21 12:20:59

Mashujaa wa mapambano dhidi ya Ebola


Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, akizungumza kwenye Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu ugonjwa wa Ebola, Jumanne tarehe 20 Januari 2015, amewapongeza wadau mbali mbali ambao wamefanya kazi kubwa, usiku na mchana huko Afrika Magharibi kwa ajili ya kuwahudumia waathirika wa ugonjwa wa Ebola na kwamba, wote hawa kwa hakika wanapaswa kutambulikana kuwa ni mashujaa dhidi ya ugonjwa wa Ebola.

Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa ni kuhakikisha kwamba, ugonjwa huu unadhibitiwa kikamilifu na kupunguza athari zake kwa waathirika, jambo linalohitaji, ukweli na uwazi.Jumuiya ya Kimataifa itaendelea kuwasaidia waathirika na kwamba, hadi sasa kuna maendeleo makubwa, juhudi za ushirikiano na mfungamano wa kimataifa.

Jumuiya ya Kimataifa kwa sasa anasema Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa inaendelea kujielekeza katika kutoa elimu na huduma za afya kwa waathirika, ili kuzuia na kudhibiti maambukizi mapya na kwamba, nchi zilizoathirika kwa ugonjwa wa Ebola zinaanza kujiandaa ili kufungua ukurasa mpya kwa kutoa huduma msingi kwa watu wake. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuendelea kusaidia harakati za maboresho ya huduma muhimu pamoja na kuwasaidia watoto yatima. Kuna haja ya kuwa na mikakati ya uhakika wa usalama wa chakula pamoja na kusaidia mchakato wa wanafunzi kuanza kurudi tena shuleni, ili kuendelea na masomo.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anakiri kwamba, ugonjwa wa Ebola kwa hakika umetikisa nguvu kazi, maisha, mapokeo, tamaduni na imani za watu. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuwekeza huko Afrika Magharibi, ili kuwaunganisha watu; kusaidia familia za wafanyakazi waliopoteza maisha wakati wakiwahudumia wagonjwa wa Ebola pamoja na kuwawezesha watu wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya huduma kwa waathirika wa ugonjwa wa Ebola.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.