Papa Francisko kuwasha moto wa Injili Barani Afrika Novemba 2015
Baba Mtakatifu Francisko wakati akiwa njiani kurejea kutoka Manila, Ufilippini, Jumatatu
tarehe 19 Januari 2015 amewaambia waandishi wa habari waliokuwa kwenye msafara wake
kwamba, anatarajia, Mungu akipenda kufanya hija ya kitume Barani Afrika kwa kutembelea
Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati na Uganda. Haya ni maeneo ambayo yamekuwa na mgogoro
wa vita kwa miaka mingi na kwamba, kuna haja ya kuanzisha tena mchakato wa amani,
upatanisho na mshikamano wa kitaifa.
Baba Mtakatifu anasema, panapomajaliwa,
hija hii ya kitume inaweza kufanyika Mwezi Novemba, 2015, wakati ambapo hakuna mvua,
ili aweze kupata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Familia ya Mungu katika nchi
hizi. Baba Mtakatifu anasema, amekuwa na wazo la kutembelea Barani Afrika, lakini
ilishindikana kutokana na kuibuka kwa ugonjwa wa Ebola, jambo ambalo lingegumisha
mkusanyiko wa makundi makubwa ya watu.
Rais Yoweri Kaguta Museven alimpotembelea
Baba Mtakatifu hivi karibuni, alipohojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican kuhusu
uwezekano wa Baba Mtakatifu Francisko kutembelea nchini Uganda kama sehemu ya mwendelezo
wa maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Mashahidi wa Uganda walipotangazwa kuwa
Watakatifu, alisema, kwamba, Vatican itatangaza hija hii kwa wakati muafaka. Alisema,
kwa mkazo kwamba, "Mambo ya wazee, wanazungumza wazee wenyewe".
Baba Mtakatifu
Francisko amekwishafanya hija ya kichungaji Barani Asia mara mbili. Kuna mamillioni
ya watu Barani Afrika yanateseka kutokana na umaskini, njaa, magonjwa, vita, kinzani
za kijamii na mashambulizi yanayofanywa na watu wenye misimamo mikali ya kidini na
kiimani. Familia ya Mungu Barani Afrika inasubiri kwa hamu na matumaini makubwa kumpokea
Baba Mtakatifu ili kuwasha tena moto wa Injili!
Na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.