2015-01-20 09:22:29

Hakuna sababu ya waamini kutunishiana misuli!


Wakristo na Waislam hawana budi kuhakikisha kwamba, wanatoa kipaumbele cha kwanza kwa mambo msingi yanayosaidia kujenga na kudumisha mshikamano na mfungamano wa kijamii; kwa kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana; kila mwamini akijitahidi kushuhudia utambulisho wake wa kidini na kitamaduni. Mauaji ya watu wasiokuwa na hatia pamoja na uharibifu wa nyumba za Ibada ni matokeo ambayo kamwe hayawezi kuvumiliwa na wapenda amani na utulivu. Si vyema watu kukashifiana katika dini na imani zao, kwani jambo hili ni hatari kwa usalama, amani na utulivu wa kijamii.

Ni changamoto inayotolewa na Askofu mkuu Claude Rault wa Jimbo Katoliki la Laghouat-Gardaia nchini Algeria kufuatia kashfa za kidini ambazo zimeendelea kusababisha maafa na uharibifu mkubwa wa nyumba za Ibada. Askofu Rault anasema, kuna haja kwa wamini wa dini mbali mbali kuheshimiana kwa kutambua na kuendeleza tunu msingi zinazowaunganisha pamoja kama taifa sanjari na kuendelea kujikita katika ujenzi wa jamii kwa kufanya kazi kwa bidii, juhudi na maarifa; kwa kuzingatia misingi ya ukweli na uwazi, kila mtu akijitahidi kutekeleza wajibu wake barabara.

Watu watambue kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Mauaji ya watu wasiokuwa na hatia kwa kisingizio cha misimamo mikali ya kidini na kiimani ni jambo ambalo linapaswa kukemea na wapenda amani wote. Watu wanategemeana anasema Askofu Rault na hakuna mtu anayeweza kuishi kama kisiwa, jambo la msingi ni kuheshimu dhamiri za watu, kutafuta na kudumisha mafao ya wengi sanjari na uhuru wa kuabudu. Hapa kama anavyosema Baba Mtakatifu kuna haja ya watu kujenga na kuimarisha madaraja ya watu kukutana na kusaidiana na wala kuta zinazowatenga watu kwa misingi ya udini, ukabila na umajimbo. Uhuru wa kuabudu, upendo na mshikamano wa kidugu ni mambo msingi katika kudumisha amani na utulivu wa kijamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.