2015-01-20 08:35:30

Athari za mabadiliko ya tabianchi ni tishio kwa maisha ya binadamu!


Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa kwamba, mkutano wa ishirini na moja wa Jumuiya ya Kimataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi, unaotarajiwa kufanyika Paris, Ufaransa Desemba, 2015, utaweza kufanya maamuzi machungu, ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Jumuiya ya Kimataifa katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabia nci ambayo yanaendelea kuwa ni chanzo cha majanga kwa nchi nyingi duniani.

Ukuaji wa mikakati ya kiuchumi si kigezo pekee cha maendeleo ya binadamu na kwamba, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuendelea kushirikiana zaidi, ili kupambana na baa la umaskini wa hali na kipato. Jumuiya ya Kimataifa ilikuwa imejiwekea Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015. Maaskofu wa Ufaransa wanasema, baadhi ya Malengo ya Maendeleo ya Millenia yamefikiwa. Lakini baa la umaskini na njaa, ni kati ya mambo ambayo hayana budi kuvaliwa njuga na Jumuiya ya Kimataifa, ili kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Kumbe, hapa kuna haja wanasema Maaskofu wa Ufaransa kujiwekea malengo ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kukuza mikakati ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa linasema, Kanisa kwa upande wake, linapenda kuwapatia watu matumaini, kwa kukazia mafao ya wengi yanayojikita katika mshikamano wa kimataifa. Ili kujenga matumaini, kuna haja ya kuwa na mwelekeo mpya wa mtindo wa maisha katika masuala ya ulaji unaowajibisha katika mchakato unaowawezesha watu kujitambua kwamba, wanahusika katika uzalishaji na utunzaji bora wa mazingira.

Maaskofu Katoliki Ufaransa wanasema, kuna haja ya kusimama kidete kulinda na kudumisha mafao ya wengi kwa kupambana kufa na kupona na athari za mabadiliko ya tabianchi zinazoendelea kusababisha umaskini mkubwa kati ya watu. Hapa kuna haja ya kuwa na sera na mikakati makini: kitaifa na kimataifa, kwa ajili ya mafao ya wengi, kwa kuongozwa na kanuni auni inayojikita katika mshikamano, ili kuwasaidia maskini kuondokana na umaskini wao. Ikumbukwe kwamba, hakuna mtu anayeweza kujitosheleza binafsi, kumbe, kuna haja ya kusaidiana ili kupambana na umaskini kama sehemu ya mchakato wa huduma kwa Familia ya binadamu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa linaendelea kuhimiza umoja na mshikamano wa kimataifa katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi sanjari na kuendelea kutekeleza Malengo ya Maendeleo ya Millenia kwa Mwaka 2015. Huu ni mchakato unaolenga kuboresha maisha ya binadamu kwa njia ya ushirikiano wa kimataifa bila kugubikwa na utaifa usiokuwa na mguso wala mashiko. Maskini washirikishwe katika mchakato wa uongozi bora, ili waweze kupanga, kuamua na kutekeleza masuala yanayohusu mustakabali na hatima ya maisha yao, kwani hata maskini wanalo jambo la kushirikisha katika ustawi na maendeleo ya binadamu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.