2015-01-19 10:40:51

TEC, Makali yako Papa Francisko tumeyaona Dodoma!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, katika Ibada ya kumsimika Askofu mkuu Beatus Kinyaiya wa Jimbo kuu la Dodoma, Jumapili tarehe 18 Januari 2015, amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwapatia heshima ya kulipandisha hadhi Jimbo la Dodoma kuwa Jimbo kuu, ili kusaidia mchakato wa kupeleka zaidi huduma za kichungaji kwa waamini, changamoto kwa Familia ya Mungu Jimbo kuu la Dodoma kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na upendo.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linaungana na Familia ya Mungu Jimbo kuu la Dodoma kumshukuru Askofu mkuu Beatus Kinyaiya kwa kukubali uteuzi wa Baba Mtakatifu Francisko wa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dodoma. Hiki ni kielelezo tosha kwamba, Baba Mtakatifu ameridhika na huduma ya kichungaji iliyokuwa inatolewa na Askofu Beatus Kinyaiya katika Jimbo Katoliki la Mbulu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linamtaka Askofu mkuu Kinyaiya kuhakikisha kwamba, anawahudumia kwa ari na moyo mkuu Watu wa Familia ya Mungu, Jimbo kuu la Dodoma, sanjari na kuendeleza na kuboresha mema yaliyoanzishwa na Wamissionari wa kwanza Jimbo Dodoma. Aendelee kuchota hekima, ujuzi na maarifa kutoka kwa watangulizi wake, ili kupambanua matatizo, changamoto na fursa mbali mbali zilizoko Jimbo kuu la Dodoma, tayari kuzifanyia kazi, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Askofu mkuu Kinyaiya atoe kipaumbele cha kwanza kwa Mungu anapotumia karama na mapaji yake katika kuwafundisha, kuwaongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu Jimbo kuu la Dodoma; daima akijitahidi kudumisha amani, upendo na mshikamano wa Familia ya Mungu, Jimbo kuu Dodoma katika ujumla wake. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema, wanahamasishwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kutoa ushirikiano wa dhati kwa Askofu mkuu Kinyaiya, ili aweze kuwatangazia maskini Habari Njema ya Wokovu kwa kuwajengea imani na matumaini!

Na Rodrick Minja,
Dodoma, Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.