2015-01-18 10:02:33

Waluteri na Wakatoliki kusherehekea kwa pamoja mageuzi ndani ya Kanisa kunako mwaka 2016


Shirikisho la Makanisa ya Kiinjili ya Kiluteri Duniani pamoja na Baraza la Kipapa linalohamasisha Umoja wa Wakristo kunako mwaka 2016, wataadhimisha kwa pamoja Jubilee ya Miaka 500 tangu mageuzi makubwa yalipofanyika ndani ya Kanisa, maadhimisho ambayo yatafikia kilele chake hapo mwaka 2017.

Kwa pamoja watashirikishana mafanikio mbali mbali yaliyokwishafikiwa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene kati ya Kanisa Katoliki na Kanisa la Kiinjili la Kiluteri. Itakumbukwa kwamba, mwaka 2017 Makanisa haya mawili yataadhimisha Jubilee ya miaka 50 ya majadiliano ya kiekumene kati ya Kanisa la Kiinjili la Kiluteri na Kanisa Katoliki.

Maadhimisho ya Mwaka 2016 yatabainisha maendeleo ya majadiliano ya kiekumene kama yanavyofafanuliwa katika hati elekezi: kutoka katika kinzani kuelekea umoja; maadhimisho ya pamoja kati ya Waluteri na Wakatoliki katika mageuzi kwa Mwaka 2017. Hati hii imeandikwa kunako mwaka 2013 kwa ushirikiano kati ya Makanisa haya mawili yanayoangalia kwa umakini mkubwa mageuzi yaliyofanyika miaka mia tano iliyopita. Hati hii inaonesha mada tete zilizojitokeza kunako karne ya kumi na sita sanjari na kubainisha maendeleo ya majadiliano ya kiekumene yaliyofikiwa hadi sasa.

Hati hii inabeba pamoja na mambo mengine, mambo makuu matano ambayo yanapaswa kufanyiwa kazi katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, ili kutoa ushuhuda wa pamoja wa Makanisa haya mawili. Kuna maelezo ya kiliturujia yanayoweza kutumiwa na Makanisa haya sehemu mbali mbali za dunia. Hii ni safari ndefu ya majadiliano ya kiekumene na kwamba, Jubilee ya miaka 500 ya mageuzi ndani ya Kanisa ni changamoto ya kiekumene anasema Mchungaji Martin Junge, Katibu mkuu wa Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani.

Kwa upande wake, Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa linalohamasisha Umoja wa Wakristo anasema, waamini wa Makanisa haya mawili, bado wanaendelea kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mwenyezi Mungu na Ukristo; hivyo, kuna hitaji la kusherehekea kwa pamoja mageuzi yaliyofanywa ndani ya Kanisa. Hii inatokana na ukweli kwamba, imani ya Kikristo inajikita katika Fumbo la Msalaba, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Kristo; mambo msingi yanayobainishwa na Luteri.

Baba Mtakatifu Francisko aliwahi kusema, kwa mara ya kwanza Waluteri na Wakatoliki wataweza kuadhimisha mchakato wa kiekumene kwa kuungama kwa pamoja katika hali ya unyenyekevu imani inayojikita katika Fumbo la Utatu Mtakatifu pamoja na kushikamana ili kupambana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.







All the contents on this site are copyrighted ©.