2015-01-17 08:27:16

Shukruni Mungu kwa kila jambo!


Baba Mtakatifu Francisko, ameianza siku ya Jumamosi, tarehe 17 Januari 2015 kwa kutembelea Jimbo kuu la Tacloban, ili kusali pamoja na kusalimiana na wahanga wa tufani ya Yolanda iliyosababisha maafa makubwa kwa wananchi wengi wa Ufilippini. Kutokana na hali ya hewa kuwa mbaya, mambo kadhaa yaliyokuwa yamepangwa kwenye ratiba ya Baba Mtakatifu yamefutwa, ili kutoa nafasi kwa Baba Mtakatifu na msafara wake kurejea tena mjini Manila.

Baba Mtakatifu katika mahubiri yake ameonesha furaha ya kuweza kuadhimisa Fumbo la Ekaristi Takatifu pamoja na wahanga wa maafa ya Yolanda yaliyokuwa na nguvu za ajabu, lakini yameshindwa kwa upendo wa Mungu, kielelezo makini cha Fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, chemchemi ya maisha na jumuiya mpya, changamoto ya kujikita katika mambo msingi yanayohudumia utu wa kila binadamu.

Baba Mtakatifu anawaomba waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kusali kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea wale wote waliofariki dunia, wale ambao bado hajawaonekana na wale walioathirika zaidi, ili Mwenyezi Mungu aweze kuwafariji kwa kuwakirimia amani ya ndani. Matukio magumu kamahaya katika maisha ya mwanadamu yanapaswa kuangaliwa kwa jicho la imani na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi, kwani hawa watafarijiwa na Mwenyezi Mungu.

Ni wajibu kwa waamini kumshukuru Mungu aliyewaangalia kwa jicho la huruma na mapendo walipokuwa katika hali ngumu ya maisha na kwamba, kwa wakati wote huu, ameweza kuwategemeza licha ya magumu yote haya ndiyo maana wanamshukuru Mungu. Baba Mtakatifu anawataka waamini kushikamana na Kristo kuhani mkuu kwani ameweza kuchukuana nao katika udhaifu wao, akajaribiwa sawasawa kama binadamu wengine katika mambo yote bila kutenda dhambi.

Kwa imani na matumaini haya anasema Baba Mtakatifu ndiyo maana waamini wanakusanyika tena kumshukuru Mungu baada ya kukumbwa na tufani ya Yolanda, katika Fumbo la Pasaka, Kristo amebeba ndani mwake, mateso na mahangaiko ya binadamu. Baba Mtakatifu anashuhudia kwamba, alipoona madhara ya tufani hii, alijisemea moyoni mwake kwamba, angalipenda kufika katika eneo hili, kuwafariji na kuwaonesha kwamba, Yesu anawapenda na kamwe hatawaacha pweke, katika shida na mahangaiko yao yote.

Waamini wayaelekeze macho yao ya imani kwenye Fumbo la Msalaba na hapo Yesu, yuko tayari kuwasindikiza tena katika hija ya maisha na wakati mwingine katika ukimya! Waamini wamkimbilie Bikira Maria katika shida na mahangaiko yao, atawaombea na kuwasaidia! Baba Mtakatifu anasema, kamwe Yesu hawezi kuwaangusha wanapomkimbilia kwa imani na matumaini makuu.

Baba Mtakatifu Francisko anawashukuru na kuwapongeza wale wote waliojisadaka kwa ajili ya kuwasaidia na kuwahudumia wahanga wa tufani ya Yolanda. Kundi lote hili ni heshima kwa Kanisa na taifa katika ujumla wake, ndiyo maana wanamshukuru Mungu kwa kila jambo, kwani ameendelea kuwa karibu nao katika shida na mahangaiko yao. Baba Mtakatifu anawashukuru wadau mbali mbali waliowasaidia wananchi wa Ufilippini kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kielelezo makini cha mshikamano wa upendo!

Bado kuna mahitaji makubwa, kumbe, kuna haja ya kuendelea kuwasaidia wananchi wa Ufilippini ili waweze kusimama tena na kuendelea na safari yao ya maisha. Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, iwasukume watu kuguswa na mahangaiko ya jirani zao pamoja na kumwachia Yesu nafasi ili aweze kuwakomboa kutoka katika ubinafsi na mapungufu yao ya kibinadamu, hasa ubinafsi.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumshukuru Mungu kwa miujiza mbali mbali ambayo amewatendea na anawaweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, msaada wa daima pamoja na maombezi ya watakatifu kutoka Ufilippini. Wote hawa wasaidia mchakato wa wananchi wa Ufilippini kujimanua kutoka katika rushwa, ufisadi na ukosefu wa haki mambo yanayochangia umaskini katika jamii.

Wakati huo huo, Askofu mkuu John F. Du wa Jimbo kuula Palo, Ufilippini, amemshukuru Baba Mtakatifu kwa kuwatembelea na kuwafariji. Amesimulia madhara yaliyofanywa na tufani ya Yolanda, lakini kwa imani na matumaini, watu wameweza kusimama tena na kuendelea na safari ya maisha, huku wakiwa wameshikamana katika umoja na upendo na kwamba, adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu ni kielelezo cha juu kabisa cha shukrani kwa Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo. Wanamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuwepo miongoni mwa maskini na waathirika wa tufani ya Yolanda!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.