2015-01-17 12:16:05

Salini ili kuombea Injili ya Uhai!


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani kuanzia tarehe 17 hadi tarehe 25 Januari 2015 linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kushiriki katika Novena kama sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Mtoto ambaye hajazaliwa, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 22 Januari, ili kukumbuka siku ile Mahakama kuu ya Marekani, kunako mwaka 1973 iliporidhia Sheria ya kutoa mimba! Tayari imekwisha gota miaka 43 tangu tukio hili lilipotokea na kuwashangaza watu wengi nchini Marekani.

Maaskofu wanasema, kuna sababu nyingi ambazo, waamini wanapaswa kuzifahamu ili kushiriki kikamilifu katika Novena ya kuombea Injili ya Uhai, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mapenzi ya Mungu. Ni nafasi ya kuonesha mshikamano wa upendo na watu wanaoteseka; kusali kwa ajili ya ustawi wa Kanisa zima, ili kweli liendelee kusimama kidete kulinda, kutetea na kutangaza Injili ya Uhai na Familia.

Hili ni tukio ambalo linapaswa kukumbukwa, kwani linasaidia watu kufahamu madhara ya kukumbatia utamaduni wa kifo. Waamini washirikiane na watu wenye mapenzi mema kwa ajili ya kusali na kutafakari, mambo msingi yatakayosaidia mchakato wa maboresho katika maisha yao ya kiroho, ili kweli waweze kuwa ni mashuhuda amini wa Injili ya Uhai miongoni mwa jamii inayowazunguka.

Maaskofu wanawaambia waamini kwamba, haitoshi tu kusali, bali kuhakikisha kwamba, wanamwilisha sala hii katika matendo kwa kukataa kukumbatia utamaduni wa kifo, ili kuheshimu kazi ya uumbaji inayotoa haki msingi kwa kila binadamu kuishi. Siku tisa za kusali kwa ajili ya kuombea Injili ya uhai ni baraka na neema kubwa kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema! Changamoto ni kusali zaidi!







All the contents on this site are copyrighted ©.