2015-01-17 10:25:37

Boresheni maisha ya maskini na imarisheni haki jamii!


Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi tarehe 17 Januari 2015 kabla ya kuzungumza na Wakleri, Watawa, Majandokasisi na wahanga wa tufani ya Yolanda kwenye Kanisa kuu la Jimbo kuu la Palo, Ufilippini, ametembelea na kufungua Kituo cha Maskini cha Papa Francisko pamoja na kusalimiana na watoto yatima, wazee na Jumuiya inayowahudumia kwa moyo wa upendo na huruma.

Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake katika mkutano huo, amewashukuru wananchi wote wa Ufilippini kutokana na ukarimu wao katika ujenzi wa maisha mapya baada ya maafa makubwa yaliyosababishwa na tufani ya Yolanda. Hiki ni kielelezo makini cha uwepo wa Mungu kati ya watu wanaoteseka na kuhangaika katika maisha pamoja na kuendelea kuwashukuru, wale wote wanaojisadaka kwa ajili ya kuwahudumia jirani zao kwa huruma na mapendo, kiasi kwamba, watu wengi wanaliona Kanisa kama alama ya matumaini mapya.

Hii ni sadaka kubwa itakayozaa matunda kwa vizazi vijavyo. Baba Mtakatifu Francisko akifanya rejea katika tukio la kubariki na kufungua Kituo cha Maskini, anasema kwamba, hiki ni kielelezo tosha kabisa cha uwepo wa Kanisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Watu wa Mungu. Hii ni changamoto kwa wanasiasa na watu wote wenye mapenzi mema, kuwasaidia, kuwahudumia na kuwaheshimu maskini katika maisha na utu wao kama binadamu.

Sera na mikakati ya kiuchumi isaidie mchakato wa maboresho ya maisha na mafao ya wengi. Ni mwaliko kwa wanasiasa kuhakikisha kwamba, wanajenga na kuimarisha haki jamii pamoja na kuwahudumia maskini badala ya kuwatenga na kuwanyanyasa!

Baba Mtakatifu kwa namna ya pekee, amewashukuru vijana walioshiriki katika tukio hili pamoja na kuonesha moyo wa upendo na ukarimu ili kuwasaidia wahanga wa tufani ya Yolanda, changamoto ya kuendeleza mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu na Utakatifu wa maisha; Hakina Amani nchini Ufilippini.

Wakati huo huo, Familia ya Mungu nchini Ufilippini imempongeza Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anapoadhimisha siku yake ya kuzaliwa. Kutokana na hali ya hewa kubadilika ghafla, Baba Mtakatifu na ujumbe wake, walilazimika kuondoka mapema huko Tacloban na hivyo kurejea tena mjini Manila na huo ukawa ni mwisho wa matukio kwa siku ya Jumamosi tarehe 17 Januari 2015.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP. S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.