2015-01-16 06:38:52

Pambaneni na changamoto za kiimani na kimaadili kwa ujasiri!


Marais wa Tume za Mafundisho Tanzu ya Kanisa waliokuwa wanafanya mkutano wao huko Esztergom, Hungaria, wamehitimisha mkutano wao uliokuwa unasimamiwa na Kardinali Gerhard L. Muller, Rais wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa, aliyesoma ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko na baadaye kufafanua kwa kina na mapana umuhimu wa Mabaraza ya Maaskofu katika urika wao wanapofundisha, ongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu.

Kardinali Muller amewakumbusha Marais hao umuhimu wa kujenga na kudumisha umoja sanjari na kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika mchakato wa kuwarithisha vijana imani na maadili mema kadiri ya mafundisho ya Kanisa. Ulikuwa ni wakati kwa wajumbe kupembua kwa kina na mapana changamoto wanazokabiliana nazo katika mikakati ya shughuli za kichungaji na kwamba, Kanisa halina budi kusimama kidete kulinda na kudumisha Injili ya Uhai.

Kardinali Muller amewakumbusha Maaskofu kwamba, wao ni walimu wa imani, inayopaswa kufundishwa na kurithishwa kwa waamini huku wakiwa wameungana na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Watambue kwamba, wokovu ni zawadi ambayo inatolewa na Kristo kwa kila mtu, kumbe ni jukumu la Kanisa Barani Ulaya kuendelea kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu. Maaskofu wamejadili pamoja na mambo mengine, nadharia, uelewa wa mafundisho ya Kanisa kuhusu binadamu; uhuru wa kidini pamoja na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika Uinjilishaji Mpya Barani Ulaya.

Wajumbe wamepembua kwa kina na mapana kuhusu umuhimu wa Sakramenti ya Upatanisho; jukumu na dhamana ya Tume ya Maaskofu kuhusu mafundisho tanzu ya Kanisa; mada ambazo zimejadiliwa katika hali ya utulivu na maelewano makubwa miongoni mwa wajumbe. Jioni ilikuwa ni nafasi ya kufahamiana na kubadilishana mawazo na mang'amuzi kuhusu mikakati ya shughuli za kichungaji Barani Ulaya. Mkutano huu imekuwa ni fursa ya kuimarisha mshikamano na umoja kati ya Tume za Maaskofu Katoliki Barani Ulaya na Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa, ili kukabiliana kikamilifu na changamoto za mafundisho tanzu ya Kanisa Barani Ulaya kwa ujasiri mkubwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.