2015-01-16 11:36:19

Jimbo kuu la Dodoma, kumekucha!


Askofu mkuu mteule Beatus Kinyaiya wa Jimbo kuu la Dodoma, Tanzania anatarajiwa kusimikwa rasmi hapo tarehe 18 Januari 2015, kadiri ya taarifa iliyotolewa na Askofu Bernadine Mfumbusa, Msimamizi wa Kitume wa Jimbo Katoliki Dodoma. Askofu mkuu mteula anatarajiwa kuwasili katika Makao Makuu ya Jimbo Katoliki Kondoa tarehe 16 Januari 2015 na kupumzika hapo akiwa anatokea Jimbo Katoliki la Mbulu.

Waamini wa Jimbo kuu Katoliki la Dodoma watampokea Askofu mkuu wa kwanza wa Dodoma hapo tarehe 17 Januari 2015 mpakani kwa Jimbo kuu la Dodoma na Kondoa. Atakapowasili Jimboni Dodoma atakabidhiwa ufunguo wa Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba na hapo masifu ya Jioni yataanza.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alilipandisha hadhi Jimbo Katoliki la Dodoma na hivyo kuwa Jimbo kuu la Dodoma linaloyajumuisha Majimbo ya Singida na Kondoa, Tanzania na kumteua Askofu Beatus Kinyaiya kuwa Askofu mkuu wa kwanza wa Jimbo kuu la Dodoma, ili kusogeza zaidi huduma za kichungaji kwa Familia ya Mungu, Kanda ya kati nchini Tanzania.

Askofu mkuu mteule Beatus Kinyaiya alizaliwa kunako tarehe 9 Mei 1957, Shimbwe, Jimbo Katoliki la Moshi. Baada ya masomo yake ya shule ya msingi, alibahatika kuchaguliwa kuendelea na masomo ya Sekondari Seminari ndogo ya Maua iliyoko Jimbo Katoliki la Moshi na baadaye akaendelea pia na masomo yake ya kidato cha tano na sita kwenye Seminari ya Itaga, iliyoko Jimbo kuu la Tabora. Baada ya masomo na majiundo yake ya maisha ya kitawa katika Shirika la Ndugu Wadogo, maarufu kama Wakapuchini, aliweka nadhiri zake za daima kunako tarehe 25 Juni 1988.

Askofu mkuu mteule Beatus Kinyaiya alisoma Falsafa Seminarini kuu ya Kibosho iliyoko Jimbo Katoliki la Moshi na kuhitimu masomo yake ya Kitaalimungu kwenye Seminari ya Mtakatifu Charles Lwanga, maarufu kama Segerea, iliyoko Jimbo kuu la Dar es Salaam. Baadaye alitumwa na Shirika kwenda kuendelea na masomo ya juu kwa kujikita zaidi katika masomo ya: historia, jiografia na falsafa huko London, Uingereza.

Baada ya kuhitimu masomo yake nchini Uingereza, alirejea tena nchini Tanzania na hapo akapangiwa kuwa ni Gombera Msaidizi na Mwalimu katika Seminari Ndogo ya Maua, iliyoko Jimbo Katoliki la Moshi, utume ambao aliufanya kati ya mwaka 1989 hadi mwaka 1992. Kuanzia mwaka 1996 hadi mwaka 1999 alikuwa ni Gombera wa Seminari ndogo ya Maua. Aliwahi kuwa ni mkuu wa Shirika la Wakapuchini nchini Tanzania na Mwenyekiti wa Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume nchini Tanzania kuanzia mwaka 1999 hadi mwaka 2005.

Baada ya kujiendeleza zaidi katika masomo ya maisha ya kiroho kutoka Chuo kikuu cha Kipapa cha Antonianum, kilichoko mjini Roma, aliteuliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Mbulu tarehe 22 Aprili 2006 na kuwekwa wakfu kuwa Askofu hapo tarehe 2 Julai 2006. Kwa ufupi, hili ndilo “Jembe jipya” la Jimbo kuu la Dodoma, Tanzania.

Tukio hili linatarajiwa kuhudhuriwa na umati mkubwa wa waamini kutoka ndani na nje ya Jimbo kuu la Dodoma.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.