2015-01-16 11:42:25

Familia ni kiota cha: Imani na Furaha!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa jioni tarehe 16 Januari 2015 amekutana na kuzungumza na Familia mbali mbali kutoka Ufilippini, kwa kuwashukuru kwa ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika maisha ya kila siku. Katika tafakari yake, Baba Mtakatifu amekazia mambo makuu matatu; kupumzika katika Kristo; kusimama na Yesu pamoja na Bikira Maria pamoja na kuendelea kuwa ni sauti ya kinabii!

Baba Mtakatifu anasema mapumziko katika Kristo ni jambo muhimu sana kwa ajili ya maisha ya kiroho na kimwili, changamoto kwa Wakristo kujenga familia na Yesu kama alivyofanya Mtakatifu Yosefu; mchakato unaopaswa kujikita kwanza kabisa katika mioyo, parokia na jumuiya zao. Kupumzika katika Kristo kunamaanisha kujenga mahusiano mema na Kristo kwa njia ya Sala, inayokuwa ni nguvu na kichocheo cha kuendelea na kazi na kamwe Wakristo wasiwe ni wavivu katika sala, vinginevyo watashindwa kutambua uwepo wa Mungu kati yao. Sala ina nafasi ya pekee katika maisha ya kifamilia.

Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, familia ni shule ya kwanza ya sala, fursa ya kukua na kufanya hija ya pamoja kama watu wa imani na kujiangalia kama sehemu ya Familia kubwa ya Mungu, yaani Kanisa. Ni shule inayowasaidia watu kujisadaka kwa ajili ya wengine, kwa kuondokana na ubinafsi na kushirikishana zawadi ya maisha na watu wengine. Hii ndiyo maana Familia ni muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anazitaka familia za Kikristo kusimama pamoja na Yesu na Maria kama alivyofanya Mtakatifu Yosefu kwa kusoma alama za nyakati, baada ya kuamka kutoka usingizini, ili kutekeleza wajibu wake. Imani haimwondoi mwamini ulimwenguni, lakini inamsaidia kuingia zaidi katika ulimwengu kwa kutenda na kusaidia mchakato wa kuandaa ulimwengu kwa ajili ya ujio wa Mungu katika utimilifu wa nyakati. Leo hii anasema Baba Mtakatifu, familia zinakabiliwa na matatizo, changamoto na kinzani nyingi.

Ufilippini ambako wamekabiliana na majanga asilia yaliyosababishwa na tufani pamoja na hali ngumu ya uchumi; ni kati ya mambo ambayo yamechangia kwa kiasi kikubwa kwa watu wengi wa Ufilippini kuhama kutoka katika nchi yao kwa kutengana na familia zao; ukosefu wa fursa za ajira na ukata katika familia nyingi ni matatizo ambayo yanaendelea kujitokeza katika maisha na utume wa familia nchini Ufilippini. Kuna kundi kubwa la familia linaloishi katika umaskini wa kutupwa, wengine wamemezwa na malimwengu kiasi hata cha kuharibu tunu msingi za maisha ya maadili, utu wema na Kikristo katika familia.

Baba Mtakatifu anazialika familia za Kikristo kujifunga kibwebwe ili kupambana na mawazo mepesi mepesi; utamaduni wa "kuganga tumbo kwa siku moja", tatizo la kutema zawadi ya maisha kwa kukumbatia utamaduni wa kifo unaopigiwa "debe" na baadhi ya taasisi mintarafu maisha ya ndoa. Mtakatifu Yohane Paulo II katika Waraka wake wa kichungaji kuhusu wajibu wa Familia za Kikristo anabainisha kwamba, ubinadamu kwa siku za usoni unarithishwa kwa njia ya familia, changamoto kwa watu kusimama kidete kusaidia familia ili kujenga jamii.

Baba Mtakatifu Francisko kwa namna ya pekee anawataka wakristo nchini Ufilippini kuimaarisha familia kwani hii ni rasilimali kwa ajili ya jamii nzima na kwamba, wito wa familia za Kikristo unarutubishwa kwa njia ya Sala, Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa na matendo ya huruma, changamoto kwa Wakristo kuhakikisha kwamba, wanatunza na kulinda familia kama Madhabahu ya Injili ya Uhai, kwa kuheshimu zawadi ya maisha, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida yanapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anazitaka familia za Kikristo kuwa kweli ni Sauti ya Kinabii kati ya watu wanaowazunguka kama alivyofanya Mtakatifu Yosefu, kwa kuwa wasikivu na makini kwa wito wa Mungu kwa Bikira Maria na Mtoto Yesu. Kwa njia hii Mtakatifu Yosefu aliweza kuingia katika Mpango wa Mungu na kuwa kweli ni baraka kwa binadamu wote.

Kwa njia ya Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu, Familia za Wafilippini hazina budi kuwa ni mfano bora wa vijana kukua katika neema, huku wakiwa makini katika tunu msingi za maisha, ili kweli waweze kuwa baraka kwa jamii nzima. Katika mantiki hii, upendo kwa Mungu unakuwa ni nguvu ya jamii na hivyo kusaidia katika mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu duniani, ili kutekeleza dhamana waliojitwalia kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo.

Baba Mtakatifu anaunganisha tabia ya kimissionari katika familia na maadhimisho ya Mwaka wa Maskini; hivyo anawaalika wananchi wa Ufilippini katika ujumla wao kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wahitaji zaidi; watu wanaokosa msingi bora wa kifamilia, wazee na watoto yatima; ambao mara nyingi wanasahaulika hata na majirani zao wa karibu. Watu hawa wahudumiwe si tu katika mahitaji yao ya kimwili, bali iwe pia ni zawadi ya kukutana na Kristo sanjari na Kanisa kama Jumuiya.

Naye Askofu Gabriel Reyes, Mwenyekiti wa Tume ya Familia, Baraza ya Maaskofu Katoliki Ufilippini anasema, kwao familia ni kiota cha furaha; mahali panapobubujika joto, lakini pia kuna baadhi yao wachenganyikiwa na kutembea katika giza; baadhi yao wamechoka na kutumbukia katika upweke hasi; kumbe maneno ya Baba Mtakatifu Francisko yamewaimarisha na kuwapatia nguvu ya kusonga mbele kwa imani na matumaini.

Familia mbali mbali nchini Ufilippini zimeshuhudia kwamba, zinadhamana ya kuendeleza utume wa familia duniani, kwa kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa kwa kuwajali na kuwahudumia maskini, huku wakitambua kwamba, wao ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.