Bahari ya Mediterania ni kaburi la wahamiaji wengi!
Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania kama sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku
ya Wakimbizi na Wahamiaji Duniani, inayoadhimishwa na Mama Kanisa hapo tarehe 18 Januari
2015, linaiomba Serikali ya Hispania kuwasikiliza kwa makini wakimbizi kabla ya kuchukua
maamuzi machungu ya kuwafukuza nchini humo.
Ni wajibu wa Serikali kuangalia
shida za wakimbizi na wahamiaji hawa ikiwa kama ni watu wanaotafuta hifadhi ya kisiasa,
au ni watu ambao ni wahanga wa vita na kinzani za kisiasa au kundi ambalo limetumbukizwa
katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo kutokana na uchu wa mali na
utajiri wa haraka haraka.
Baada ya kuangalia sababu zote hizi, hapo Serikali
inawajibu wa kutekeleza sheria za kimataifa mintarafu wahamiaji na wakimbizi, vinginevyo
ni kutowatendea haki watu hawa ambao wanakumbana na majaribu makubwa katika maisha
yao. Kwa kuwasikiliza kwa makini anasema Askofu Ciriaco Benavente wa Jimbo Katoliki
Albacete, Hispania, Serikali inaweza kufanya maamuzi ya haki na usawa.
Inasikitisha
kusema kwamba, Bahari ya Mediterania kwa sasa imekuwa ni kaburi kuu la wahamiaji na
wakimbizi wanaokimbia nchi zao kutokana na sababu mbali mbali, kwa matumaini ya kupata
maisha bora, lakini wanajikuta wakimezwa na kufukiwa kwenye Bahari ya Mediterania
na huo ndio unakuwa ni mwisho wa ndoto ya maisha bora zaidi. Hispania na Italia kwa
sasa ni kati ya nchi ambazo zinapokea idadi kubwa ya wahamiaji na wakimbizi na taarifa
zinazonesha kwamba, zaidi ya watu 3, 000 wamekufa maji huko Hispania na kati yao kuna
watoto 15.
Takwimu zinaonesha kwamba, Hispania inatoa hifadhi kwa wakimbizi
na wahamiaji millioni 5. Askofu Benavente amewakumbusha wananchi wa Hispania ambao
wamesahau kwamba, hata Jamii kubwa ya Hispania ni watoto wa wahamiaji na wakimbizi,
kumbe wanapaswa kuguswa na mahangaiko ya watu hawa badala ya kuwatelekeza katika shida
na mahangaiko yao!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.