Ujumbe kwa Siku ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani kwa Mwaka 2015
Kanisa bila mipaka kwani ni mama wa wote ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Baba
Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Siku ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani,
inayoadhimishwa na Mama Kanisa tarehe 18 Januari 2015. Mama Kanisa anahamasishwa kuhakikisha
kwamba, anafungua mikono yake ili kuwakaribisha watu wote bila ubaguzi wala kikomo.
Baba Mtakatifu
anasema, Yesu Kristo ndiye Mwinjilishaji mkuu, aliyeonesha upendeleo mkubwa kwa watu
waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii, anwaalika waamini na watu wote wenye
mapenzi mema kuwahudumia wale wanaosumbuka na kuteseka, kwa kutambua ndani mwake mateso
ya watu wanaotumbukizwa katika mifumo mipya ya umaskini na utumwa, kwa njia ya matendo
ya huruma.
Kanisa katika utume wake, linatambua kwamba ni hujaji hapa ulimwenguni
na Mama wa wote, hivyo linahamasishwa kumpenda na kumwabudu Yesu Kristo anayejionesha
kati ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, kati yao ni: wahamiaji
na wakimbizi, wanaotafuta nafuu ya maisha kwa kukimbia magumu wanayokabiliana nayo.
Ndiyo maana anasema Baba Mtakatifu Francisko, kauli mbiu ya maadhimisho ya Siku ya
Wahamiaji na Wakimbizi kwa mwaka huu ni “Kanisa bila mipaka, Mama wa wote”.
Kanisa
linafungua mikono yake na kuwakaribisha watu wote bila ubaguzi au kikomo, ili kuwatangazia
kwamba, Mungu ni upendo. Yesu Kristo mara baada ya kufufuka kwake aliwakabidhi wafuasi
wake utume wa kushuhudia na kutangaza Injili ya Furaha na Huruma. Siku ile ya Pentekoste,
mitume walijitokeza hadharani, wakiwa wameimarishwa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu wakashinda
woga na mashaka yaliyokuwa yamejikita mioyoni mwao na wote waliosikia Habari Njema
ikitangazwa masikioni mwao, wakaelewa ujumbe huo katika lugha zao wenyewe.
Tangu
mwanzo, Kanisa limekuwa ni Mama ambaye moyo wake uko wazi na bila mipaka. Utume huu
umeendelezwa kwa takribani miaka elfu mbili sasa. Tangu mwanzo, Wamissionari walitangaza
na kushuhudia Umama wa Kanisa, dhana ambayo iliendelezwa na Mababa wa Kanisa na kufanyiwa
kazi kwa umakini zaidi na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, walipotamka kuwa
Kanisa ni mama, Ecclesia Mater, ili kufafanua asili ya Kanisa linalowakumbatia
wote moyoni mwake kwa njia ya upendo.
Kanisa mama wa wote pasi na mipaka, limeenea
sehemu mbali mbali za dunia, ili kuendeleza utamaduni wa ukarimu na mshikamano kwa
kutambua thamani ya kila binadamu. Kanisa linapoishi kikamilifu dhana hii ya umama,
Jumuiya za Kikristo zinarutubishwa, zinaelekeza na kuonesha njia, zinawasindikiza
watu kwa uvumilivu na kuwakumbatia kwa njia ya sala na matendo ya huruma.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, yote haya yanapata maana mpya kutokana na ukweli kwamba,
kuna wimbi kubwa la wahamiaji linalokimbia nchi zao, wakiwa wamebeba masanduku ya
woga na matumaini wakiwa tayari kuanza safari ya matumaini, lakini inayosheheni hatari,
ili kutafuta maisha bora zaidi. Kwa bahati mbaya, wahamiaji hawa wanakumbana na hali
ya kinzani hata katika Jumuiya za Kikanisa bila hata ya kujitaabisha kufahamu historia
ya madhulumu na hali ya kukatisha tama.
Ni watu wanaoangaliwa kwa “jicho la
kengeza”, wanaotiliwa mashaka kiasi hata cha kuweka kando Amri ya Maandiko Matakatifu
inayowataka waamini kuwakaribisha kwa heshima na mshikamano wageni wenye shida. Kutoka
katika undani wa dhamiri nyofu, waamini wanahimizwa kugusa mateso na mahangaiko ya
wahamiaji ili kuwaonjesha amri ya upendo ambayo Yesu amewaachia wafuasi wake. Wageni
hawa ni wale wanaoteseka, wahanga wa madhulumu na unyonyaji; wote hawa waonjeshwe
ukarimu wa Kristo kama njia ya kuendelea kuganga madonda ya Yesu.
Baba Mtakatifu
Francisko anasema, ujasiri unaoibuliwa kutoka katika imani, mapendo na matumaini inawawezesha
waamini kupunguza umbali uliopo kati yao na umaskini wa watu. Yesu anasubiri kutambuliwa
kati ya wahamiaji na wakimbizi; kati ya wale wanaoteseka na kunyanyasika ugenini na
kwa njia yao, Yesu anawahamasisha wafuasi wake kuwashirikisha rasilimali pamoja na
kuwamegea kidogo, utajiri ambao Mwenyezi Mungu amewakirimia katika maisha yao, ili
uweze kutumika kwa ajili ya mafao ya wengi kama anavyokazia Mwenyeheri Papa Paulo
VI.
Jamii mamboleo inajionesha katika tamaduni mbali mbali. Ndiyo maana Mama
Kanisa anawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujikita katika mshikamano,
umoja na uinjilishaji. Makundi ya wahamiaji ni changamoto kwa Kanisa kuhakikisha kwamba,
linakuza na kuimarisha tunu msingi zitakazodumisha amani na utulivu kati ya watu na
tamaduni. Watu wenye tamaduni na asili tofauti wanapaswa kuheshimiana, kwa kuvunjilia
mbali tabia ya watu kujikita katika woga usiokuwa na mashiko na kutaka kujilinda wenyewe
kwa kutowajali wakimbizi na wahamiaji. Mama Kanisa anahamasisha utamaduni wa watu
kukutana, ili kujenga dunia iliyo bora zaidi inayojikita katika haki na udugu.
Makundi
makubwa ya wahamiaji yanayoendelea kujitokeza katika uso wa dunia anasema Baba Mtakatifu,
yanahitaji ushirikiano wa dhati kati ya Serikali na Mashirika ya kimataifa, ili kudhibiti
na kuratibu mwenendo wa wahamiaji na wakimbizi kwa ufanisi zaidi mintarafu masuala
ya: kijamii, kiuchumi, kisiasa, kitamaduni na kidini sanjari na matatizo na changamoto
zote zinazoweza kujitokeza katika masuala kama haya kitaifa na katika ngazi ya Kimataifa.
Katika
ngazi ya Kimataifa kumekuwepo na mijadala inayogusia wajibu, mbinu na sheria zinazoweza
kutumika kwa ajili ya kudhibiti wimbi la wahamiaji na wakimbizi, huduma inayotolewa
na wadau katika ngazi mbali mbali, lakini utekelezaji wa sera na mikakati hii yamebaki
kuwa ni maneno matupu kuliko vitendo, changamoto ya kutekeleza sera hizi kwa njia
ya ushirikiano wa kimataifa, kwa kuheshimu utu na mwanadamu akipewa kipaumbele cha
kwanza. Hali hii itasaidia kwa kiasi kikubwa kupambana na biashara haramu ya binadamu
ambayo ni uhalifu dhidi ya ubinadamu, inayowapoka watu haki zao msingi kwa kuwatumbukiza
katika mateso, dhuluma na utumwa.
Baba Mtakatifu anasema, ushirikiano wa pamoja
unahitaji kujikita katika umoja, kwa kubainisha mbinu mkakati shirikishi, ukweli na
uwazi, kwani hakuna nchi ambayo inaweza kujigamba kwamba inaweza kukabiliana na tatizo
la wahamiaji na wakimbizi kwa jeuri yake yenyewe. Uhamiaji wa utandwazi unaweza kudhibitiwa
kwa kujikita katika utandawazi wa upendo na ushirikiano ili kuboresha hali ya maisha
ya wakimbizi na wahamiaji duniani, sanjari na kuhakikisha kwamba, mambo yote yanayosababisha
watu kuzikimbia nchi zao yanadhibitiwa kikamilifu. Sababu kubwa ni vita na njaa; mambo
yanayowalazimisha watu kuzikimbia nchi zao.
Baba Mtakatifu anasema, mshikamano
na wahamiaji pamoja na wakimbizi hauna budi kusindikizwa na ujasiri pamoja na kipaji
cha ugunduzi, kinachoweza kutekelezwa katika ngazi ya kimataifa kwa kudumisha haki
na usawa katika masuala ya fedha na uchumi na kuendelea kujikita katika mchakato wa
kujenga na kudumisha amani, kichocheo kikuu cha maendeleo endelevu ya watu.
Baba
Mtakatifu Francisko anawaambia wahamiaji na wakimbizi kwamba, wao wanayo nafasi ya
pekee katika moyo wa Kanisa na kwamba, wanalisaidia Kanisa kuonesha umama wake kwa
familia ya binadamu. Anawataka kukuza na kudumisha imani na matumaini, kwa kutambua
ujasiri wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu iliyolazimika kukimbilia Misri,
ili kuokoa maisha ya Mtoto Yesu. Kwa hakika Mwenyezi Mungu hataweza kuwaacha katika
shida na mahangaiko yao kama alivyofanya kwa Familia Takatifu.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.