Papa Francisko awasha cheche za matumaini nchini Sri Lanka!
Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko, Jumatano tarehe 14 Januari 2015 ametembelea Hekalu la Wabudha, akakutana
na Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka pamoja na kuzungumza na Rais wa zamani wa
Sri Lanka aliyekuwa ameambatana na familia yake!
Itakumbukwa kwamba, Rais mstaafu
Mahinda Rajapaksa ndiye aliyekuwa amemwalika rasmi Baba Mtakatifu Francisko kutembelea
nchini Sri Lanka, lakini siku chache tu kabla ya kuwasili kwa Baba Mtakatifu nchini
humo akashindwa kwenye uchaguzi mkuu.
Baba Mtakatifu amemshukuru kwa maandalizi
mazuri yaliyofanikisha hija yake ya kitume nchini Sri Lanka, lakini kwa namna ya pekee,
amani, utulivu, umoja na mshikamano wa kitaifa uliojionesha mara baada ya matokeo
ya uchaguzi mkuu kutangazwa rasmi. Tukio hili limeonesha ukomavu wa kisiasa na kidemokrasia
nchini Sri Lanka.
Padre Lombardi anasema, Baba Mtakatifu ametembelea Hekalu
la Kibudha na kusalimiana na viongozi wake wakuu, akapewa maelezo ya kina kuhusiana
na nyumba hii ya sala, inayofunguliwa mara moja kwa mwaka. Wakati huu, Hekalu hili
lilifunguliwa kwa heshima ya Baba Mtakatifu Francisko, kama kielelezo cha heshima,
upendo na urafiki katika mchakato wa majadiliano ya kidini unaofumbatwa katika utamaduni
wa watu kukutana.
Baba Mtakatifu aliweza kukutana na kuzungumza na Baraza la
Maaskofu Katoliki Sri Lanka kwenye Makao makuu ya Jimbo kuu la Colombo. Baba Mtakatifu
amebadilishana mawazo na Maaskofu katika hali ya urafiki na upendo mkuu. Kutokana
na matatizo ya usafiri kutoka kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu
Madhu, Maaskofu walichelewa kidogo, lakini Baba Mtakatifu aliwasubiri na baadaye akazungumza
nao kwa kukazia umuhimu wa Padre Joseph Vaz kutangaza kuwa Mtakatifu na kwamba, atasaidia
kukoleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya nchini Sri Lanka, unaojikita katika majadiliano
ya kidini, haki, amani na upatanisho.
Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru
kwa namna ya pekee, wananchi wa Sri Lanka kwa kumpatia hundi ya dolla za kimarekani
sabini elfu, ili kuwasaidia maskini na wote wanaohitaji msaada na huruma ya Baba Mtakatifu..
Padre Lombardi anasema, Mwenyeheri Paulo VI na Mtakatifu Yohane Paulo II wakati
wa hija zao za kichungaji nchini Sri Lanka hawakubahatika kutembelea na kusali kwenye
Madhabahu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu wa Madhu, kielelezo cha upatanisho, umoja
na mshikamano wa kitaifa. Kumbe, Baba Mtakatifu Francisko ametembelea na kusali katika
Madhabahu haya yanayopendwa na waamini kutoka katika dini mbali mbali nchini Sri Lanka.
Hapa wanajisikia kupendwa, kuthaminiwa na kuheshimiwa.
Katika Madhabahu haya,
Baba Mtakatifu ametafakari kwa kina kuhusu umuhimu wa upatanisho, toba na msamaha
wa kweli, ili kuvuka kinzani na migawanyiko inayotokana na tofauti za kidini, kisiasa,
kitamaduni na kikabila. Baba Mtakatifu amepokea Sanamu ya Bikira Maria na kuwabariki
watu waliokuwa wamefurika katika Madhabahu haya.
Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu
imechangia mchakato wa amani, umoja na mshikamano wa kitaifa, tayari kuendeleza upatanisho
wa kitaifa. Kanisa Katoliki nchini Sri Lanka limeonesha umahiri mkubwa katika kuandaa
na kutekeleza hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu nchini humo na kwamba, Baba Mtakatifu
ameridhika na mapokezi makubwa yaliyofanywa kwake, jambo ambalo limewasha cheche za
matumaini.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.