2015-01-15 09:27:14

Changamoto kubwa ni kuendeleza majadiliano ya kidini, maridhiano, haki na amani!


Kardinali mteule Charles Maung Bo, Askofu mkuu wa Yangon, nchini Myanmar, atakaposimikwa rasmi, hapo tarehe 14 Februari 2015, atakuwa ni Kardinali wa kwanza kutoka nchini humo. Anasema, changamoto kubwa inayomkabili mbele yake ni kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini, maridhiano, haki na amani kati ya wananchi wa Mynmar. RealAudioMP3

Kanisa Katoliki nchini humo linawakilisha idadi ndogo sana ya wananchi wa Mynmar na kwamba, kwa sasa nchi yake iko katika kipindi cha mpito kuelekea kukua kwa demokrasia baada ya utawala wa mabavu kutikisa nchi hiyo kwa miaka kadhaa. Kinzani za kisiasa zilipelekea kuibuka kwa mgogoro wa kidini na kikabila, hali ambayo imesababisha kurasa chungu kwa wananchi wa Myanmar.

Viongozi wa kidini anasema Kardinali mteule Bo, wanaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kujenga msingi wa haki, amani, upatanisho na maridhiano kati ya watu na kwamba, anapenda kuchukua fursa hii kuhakikisha kwamba, viongozi wa kidini wanashrikiana kwa karibu zaidi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu wao.

Ukosefu wa haki msingi za binadamu na utawala wa sheria ni mambo ambayo yanapelekea kwa kiasi kikubwa uwepo wa kinzani za kidini na kikabila, kwani kuna kundi la watu ambalo linaona kwamba, halitendewi haki kama inavyostahili kadiri ya Katiba ya nchi ambayo kimsingi ni sheria mama. Kwa sasa kuna muswada wa sheria ambao una taka kuzuia masuala ya ndoa na uhuru wa kidini: changamoto kubwa katika kudumisha amani na utulivu!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.