2015-01-14 07:54:18

Mtakatifu Joseph Vaz, Utuombee!


Kardinali Malcolm Ranjith wa Jimbo kuu la Colombo, Sri Lanka anasema, Mtakatifu Joseph Vaz alizaliwa huko Goa, Hindia kunako tarehe 21 Aprili 1651, hata katika ujana wake, ni mwamini aliyejipambanua kwa maisha ya sala na tafakari ya kina, kwa kutumia muda wake mwingi kwa ajili ya sala. RealAudioMP3

Alikuwa ni msomi, aliyejisadaka kwa ajili ya kuwahudumia maskini na wote waliokuwa wanasukumwa pembezoni mwa jamii; kwa kuwaoneha huruma na upendo wa Mungu katika hali ya unyenyekevu pasi na makuu; alikuwa ni mtu wa furaha katika kuwahudumia watu; mambo yaliwagusa watu kutoka katika undani wao, wengi wakauona utakatifu wa maisha yake tangu awali.

Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikuhani, akapewa Daraja takatifu la Upadre kunako mwaka 1676 akiwa ni Padre wa Jimbo kuu la Goa, India. Lakini ndani mwake, aliendelea kujisikia kuwa na wito wa kuwa Mmissionari, tayari kutoka ili kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu, akamua kujiunga na na Shirika la Padre Pasqual dal Costa Jeremias; baadaye akawa ni kiongozi na hatimaye wakajiunga na Shirika la Mtakatifu Filippo Neri. Akiwa Jimbo kuu la Goa, akaanzisha Shirika lake binafsi, kwa kuendeleza sheria na kanuni za Shirika la Mtakatifu Filippo Neri.

Padre Joseph Vaz alibahatika kufahamu kwa undani mateso na mahangaiko ya Wakristo nchini Sri Lanka na kunako mwaka 1687 akaamua kwenda nchini humo kama mfanyakazi. Haikuwa rahisi kwake kukutana na Waamini wa Kanisa Katoliki, lakini aliendelea kujifunza lugha ya kitamil, akahudumia waamini katika hali ya kificho na baadaye Waholanzi walimshtukia na kuanza kumtafuta kwa udi na uvumba, ili wapate kumwadabisha, kwani walimshutumu kuwa ni mpelelezi wa Wareno waliokuwa wanatawala eneo hili kwa nyakati zile.

Siku moja akiwa njiani kwenda kukutana na Mfalme wa kitongoji cha Kandy, alikamatwa na kutiwa kizuizini. Baada ya miaka miwili aliachiliwa na kupewa kifungo cha nje na hivyo kuendelea na utume wake kama mchungaji na kiongozi wa maisha ya kiroho, akachakarika kuwatangazia Watu Habari Njema ya Wokovu sanjari na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa; akaonesha matendo makuu ya Mungu katika maisha yake, kwa kufanya miujiza.

Alikataa katu katu alipoombwa kuwa Askofu, akataka aendelee kuhudumia kama Padre. Mateso aliyopata awali na kuyakubali kwa moyo wa unyenyekevu yalimsababishi maradhi makubwa na tarehe 16 Januari 1711 akafariki dunia! Ni Padre aliyejisadaka na kumwachia Kristo aweze kuyaongoza maisha yake kama alivyokuwa Yohame Mbatizaji katika Agano Jipya. Kunako mwaka 1713 cheche za mchakato wa kumtangaza Padre Joseph Vaz kuwa Mwenyeheri zikaanza huko Goa na Kandy.

Kunako mwaka 1989 Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu likatambua ushuhuda wake wa imani na miujiza iliyotendwa kwa maombezi yake. Papa Yohane Paulo II tarehe 21 Januari 1995 akatangaza kuwa ni Mwenyeheri, wakati wa hija yake nchini Sri Lanka.

Waamini na watu wenye mapenzi mema kutoka ndani na nje ya Sri Lanka waliendelea kusali kwa maombezi ya Mwenyeheri Joseph Vaz na Baba Mtakatifu Francisko kunako tarehe 20 Oktoba 2014 akaamua atangazwe kuwa Mtakatifu, tukio ambalo linafanyika nchini Sri Lanka wakati wa hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko. Kanisa linafurahi kwa kupata zawadi hii kubwa na linamshukuru kwa kuwaimarisha waamini katika imani na kwamba, ataendelea kukumbukwa kama mmissionari hodari aliyejisadaka kwa ajili ya kuwatangazia watu Injili ya Matumaini kwa Kristo na Kanisa lake.

Sri Lanka ikawa ni chachu ya Uinjilishaji Barani Asia, kwa kuwa ni mahali pa kwanza kabisa Barani Asia kuwa na Seminari kwa ajili ya majiundo ya Majandokasisi mahalia, tayari kujisadaka kwa ajili ya kuwatangazia watu Injili ya Kristo. Papa Leo mkuu, aliwahamasisha viongozi wa Kanisa kuhakikisha kwamba, wanawafunda waseminari kikamilifu, tayari kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji wa watu Barani Asia.

Ukuu wa Mwenyeheri Joseph Vaz unafumbatwa katika maamuzi yake ya kujisadaka kwa ajili ya upendo na huduma kwa ndugu zake katika Kristo waliokuwa wanateseka bila ya kuwa na mchungaji; ni mwamini aliyejiachilia mikononi mwa Mungu, kwa ajili ya huduma kwa maskini; akaonesha ukuu wa maisha ya sala na tafakari ya Neno la Mungu; akaadhimisha Mafumbo Matakatifu kwa Ibadan a moyo mkuu, chemchemi ya utakatifu wa maisha na ukuu wa Mungu kwa watu wake. Kwa hakika ni Joseph Vaz ni Mmissionari wa kuigwa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya, changamoto kubwa inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Wakristo Barani Asia hawana wasi wasi tena wa kuteseka kutokana na umaskini wala madhulumu, wanachohitaji ni Wamissionari wanaojisadaka kwa ajili ya kuwatangazia watu Injili ya Furaha na Matumaini kwa Kristo na Kanisa lake, ili Kristo aendelee kufahamika pasi na makuu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.