2015-01-13 10:06:53

Ukabila na Umajimbo yamepitwa na wakati!


Askofu Paul Abel Mamba wa Jimbo Katoliki Ziguinchor, Senegal anasema, watu wanasubiri kwa hamu na shauku kubwa mchakato wa amani utakaowawajibisha wahusika wa vurugu na kinzani nchini Senegal kuweka silaha zao chini na kuanza majadiliano katika ukweli, uwazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Senegal.

Tangu mwaka 1982 kuna makundi yanapigana huko Casamance ili kujitenga na Senegal. Askofu Paul Abel Mamba katika salam na matashi mema ya Mwaka mpya 2015 alizowaandikia viongozi wa Serikali katika Jimbo lake, amewataka viongozi hao kuhakikisha kwamba, amani, utulivu na maendeleo ya wengi huko Casamance yanapewa kipaumbele cha kwanza katika ajenda za kisiasa kwenye ngazi ya kitaifa kwa mwaka 2015.

Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, makundi haya anasema Askofu Mamba yameendelea kukwamisha mchakato wa majadiliano ili kupata amani ya kudumu. Kwa sasa hakuna vita wala watu hawana uhakika wa usalama wa maisha na mali zao. Umefika wakati kwa wadau wakuu kuachana na ubinafsi, uchu wa mali na madaraka, ili kutoa kipaumbele cha kwanza kwa amani, utulivu sanjari na ujenzi wa umoja na mshikamano wa kitaifa kwani ukabila na umajimbo ni mambo ambayo yamepitwa na wakati kwa sasa!







All the contents on this site are copyrighted ©.