Baba Mtakatifu Francisko, akiwa njiani kuelekea Sri Lanka na Ufilippini wakati wa
ziara yake, aliyoianza Jumatatu usiku, tarehe 12 Januari 2015, amewaandikia ujumbe
wa matashi mema marais wa Italia, Albania, Ugiriki, Uturuki, Iran, Umoja wa Falme
za Kiarabu, Oman na India.
Baba Mtakatifu amewatakia wakuu hao wa nchi pamoja
na wananchi wao amani, usalama na ustawi sanjari na kuwapatia baraka zake za kitume.
Amewahakikishia Marais hao sala na maombezi yake na kuwaomba hata wao kumsindikiza
kwa sala na sadaka zao katika hija yake ya kitume huko Sri Lanka na Ufilippini. Baba
Mtakatifu anawatakia wananchi wote ambao ndege yake imebahatika kuruka katika anga
lao, amani na furaha.
Kwa namna ya pekee, amewaambia wananchi wa Uturuki kwamba,
bado moyoni mwake kuna kumbu kumbu ya hija ya kichungaji aliyoifanya nchi mwao hivi
karibuni na kwamba, bado anaendelea kuwakumbuka kwa sala! Baba Mtakatifu amewatakia
wananchi wa Iran, Falme za Kiarabu na Omani, amani na ustawi, kama ambavyo pia amefanya
kwa Rais wa India.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.