2015-01-10 08:30:38

Vitendo vya kigaidi!


Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa amesikitishwa na mauaji ya kinyama yanayoendelea kufanywa na Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram nchini Nigeria kwa kusema kwamba, kuna haja ya kujikita katika majadiliano yanayosimikwa katika ukweli na uwazi; watu kuvumiliana katika tofauti zao za kidini, kisiasa, kijamii na kitamaduni; kwa kukazia ulinzi na usalama kwa watu na mali zao sanjari na kuendelea kuelimisha tabia ya uungwana kati ya watu. RealAudioMP3

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema, ni kwa njia hii, tu, Jumuiya ya Kimataifa itaweza kupambana vyema na changamoto ya vitendo vya kigaidi ambavyo vinaendelea kutishia usalama, maisha, ustawi na maendeleo ya watu sehemu mbali mbali za dunia. Dunia bado imepigwa na bumbuwazi kutokana na mauaji ya kinyama yanayofanywa huko Iraq, Syria, Libia na Ufaransa. Viongozi wa kidini wasimame kidete kupinga mauaji ya kinyama yanayofanywa na waamini wenye misimamo mikali ya kiimani, kwani watu hawa ni hatari kwa usalama wa Jumuiya ya Kimataifa.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa katika kikao cha Baraza kuu la Umoja wa Mataifa ameitaka Jumuiya ya Kimataifa kujikita katika majadiliano na maridhiano kati ya watu, ili kujenga na kuimarisha haki, amani na mshikamano, ili kushinda kishawishi cha vitendo vya kigaidi ambavyo vinaendelea kuzua hofu na mashaka kati ya watu. Jumuiya ya Kimataifa inaweza kulinda na kudumisha amani na utulivu, ikiwa kama haki msingi za binadamu zinaheshimiwa na kuthaminiwa, bila kusahau uhuru wa kidini.

Wachunguzi wa mambo ya kisiasa wanasema mashambulizi ya kigaidi yanayofunikwa kwa blanketi la misimamo mikali ya kidini, lakini nyuma yake kuna masilahi ya kiuchumi, yanayochochewa sana na biashara haramu ya silaha ambayo imekuwa ni chanzo kikuu cha vita na majanga yanayoendelea kutokea sehemu mbali mbali za dunia.

Ugaidi ni jambo linalotishia maisha, usalama, ustawi na maendeleo ya watu, jambo ambalo kwa sasa linavaliwa njuga na viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa. Jambo la kushangaza ni kuona kwamba, kuna idadi kubwa ya wananchi kutoka katika nchi za Ulaya wanaojiunga na vikundi vya kigaidi ili kufanya mashambulizi si tu katika nchi za kigeni hata katika nchi zao asilia. Jumuiya ya Kimataifa inaendelea kuchukua tahadhari kubwa kuhusiana na vitendo vya kigaidi.









All the contents on this site are copyrighted ©.