2015-01-08 09:46:36

Shetani tokaaa!


Huu si mchapo ni Neno! "Mara akatokea mle ndani ya Sinagogi mtu mmoja mwenye pepo mchafu, akapaza sauti, 'Una nini nasi, wewe Yesu wa Nazareti? Je, umekuja kutuangamiza? Najua wewe ni nani: wewe ni Mtakatifu wa Mungu!' Yesu akamkemea huyo pepo akisema, 'Nyamaza! Mtoke mtu huyu'. Basi, huyo pepo mchafu akamtikisatikisa mtu huyo, kisha akalia kwa sauti kubwa, akamtoka. (Marko 1:23-26).

Hapa tuona nguvu ya Yesu katika kugusa na kurekebisha maisha yetu. Yesu huyo ambaye hivi karibuni tumempokea katika maadhimisho ya Noeli na kusema "Mtoto amezaliwa kwa ajili yetu, tumepewa mtoto mwanaume mwenye uweza wa kifalme mabegani mwake".

Huyu ndiye Yesu aliyejidhihirisha kwa Mamajusi kutoka Mashariki ya Mbali, waliomtambua na kumsujudia, huku wakimtolea zawadi zao. Yesu ni mfalme wa amani, matumaini na mapendo; ni Mfalme mwenye uweza mkuu kwa hiyo tusiishie kumkaribisha tu kwa maneno, kwa nyimbo, kwa kumlia pilau na kumnywea soda na “viroba” Wala siyo kwa kumvalia nguo mpya kama tufanyavyo tunaposherekea kuzaliwa kwa Yesu, bali tumkaribishe kwa dhati maishani mwetu ili asafishe tabia zetu chafu ambazo sisi zimetushinda na tumezizoea na kuzifanya sehemu muhimu ya maisha yetu.

Tabia hizo mbaya ndiyo pepo wachafu ambao wao wanamtambua Yesu na wanatambua uweza wake, wanamwogopa. ulevi, ulafi, uzinzi, uongo, uvivu, chuki, hasira, kukata tamaa, nguvu za giza, kutokushiriki mambo matakatifu, unafiki, undumilakuwili, kutokuwatendea haki wenzetu, rushwa, kupenda anasa na fahari zote za kishetani, kutotimiza wajibu na nyingine nyingi ni pepo wachafu ambao sisi tumewapa nafasi katika maisha yetu ya kila siku, ni tabia ambazo zimetuzoea hatuna nguvu nazo. Ni tabia ambazo zinatufarakanisha katika familia zetu, makazini na katika jamii.

Hizi ni tabia ambazo badala ya kutupa furaha zimekuwa karaha kwetu, hatuna uwezo nazo, zinatuendesha. Leo tunapata jibu, huyo mfalme mwenye uweza ndiye jibu kubwa, tuzitafakari tabia zetu, ambazo zinatukosesha malengo yetu na zinatukosesha pia ya mbingu. Nguvu hizi za pepo wachafu hazina nguvu mbele ya Yesu.

Tumuombe huyu 'mtoto aliyezaliwa kwa ajili yetu' ili atuondolea 'mizigo hiyo' inayotuelemea katika maisha yetu ili tuanze vyema mwaka huu tukiwa bila pepo wachafu.

Tumsifu Yesu Kristo!
Na Antipasi Shinyambala,
Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.