2015-01-08 09:27:07

Maimamu wa Kifaransa mjini Vatican, ishara ya urafiki na majadiliano


Watu sita walionusurika katika kambi za mateso ya Auschwitz na maimamu wanne toka Ufaransa, walikuwa kati ya umati mkubwa wa watu waliohudhuria katekesi ya Papa Francisko , Jumatano ya wiki hii mjini Vatican. Kukutana kwao na Papa kumetajwa kuwa ushuhuda dhahiri wa Wakatoliki na Waislamu, kupania kutembea pamoja katika hatua za kujenga urafiki na maelewano, kama haja ya kidharura kwa ajili ya udumishaji amani na dhamira ya kupambana na unyanyasaji wowote.

Maimamu hawa wanne, ni wajumbe wa miaka mingi katika vikao vya pamoja vya Wakatoliki na Waislamu nchini Ufaransa, vikao vyenye kuwa na lengo la kufanya kazi wa ushirikiano, kwa ajili ya kukuza majadiliano halisi kati ya Wakatoliki na Waislamu. Ameeleza Askofu Michel Dubost wa Jiobo la Evry-Corbeil –Essonnes , ambaye ni Mwenyekiti wa Tume ya Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa kwa ajili ya Mahusiano na Madhehebu mengine. Anasema, kufahamiana husaidia kujenga mahusiano ya kirafiki na hivyo hurahisisha kupata majawabu yanayofaa panapojitokeza changamoto ngumu, kati ya waamini wa dini hizi mbili.

Na ameitaja ziara ya uwakilishi huu wa Waislam kutembelea Vatican , kuwa si kitendo cha kipekee, lakini ni ishara nzuri ya utendaji wa kazi zao za pamoja kwa ajili ya ujenzi wa amani. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa uwakilishi wa juu wa Waislamu wa Ufaransa, kukutana na Papa Francisco. Na kwamba, kazi za majadiliano yao, hulenga kuwaongoza katika njia ya kupata majawabu, hasa jinsi ya kushughulikia mizizi ya ubabe wa kupindukia wa kidini, uzuri wa kuvumiliana , na kujaribu kutoa majibu kwa mvutano wa kutisha unapojitokeza kati ya madhehebu na dini, hali inayoonekana sehemu nyingi za Ulaya, lakini pia suala nyeti Mashariki ya Kati.

Askofu Dubost aliwatambulisha Maimmu hao kwa Papa. Nao ni Azzedine Gaci, gombera wa msikiti Orhman wa Villeurbanne, Maalim Tareq Oubrou, gombera wa Msikiti Mkuu wa Bordeaux, mwingine ni Mohammed Moussaoui rais wa Umoja wa misikiti nchini Ufaransa, na Djelloul Seddiki ambaye ni mkurugenzi wa Msikiti Mkuu wa Al Ghazali wa Paris. Pamoja nao alikuwepo pia Padre kuhani Christophe Roucou, Mkurugenzi katika Tume ya Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa kwa ajili ya mahusiano na Uislamu.

Ujumbe huu wa Kiislam toka Ufaransa umekuwa Roma kwa ajili ya kushiriki katika mfululizo wa mikutano ya ngazi ya juu, inayokamilika Alhamisi hii 8 Januari 2015, kwa kukutana na Kardinali Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Majadiliano ya kidini.











All the contents on this site are copyrighted ©.