2015-01-06 10:00:57

Utakatifu wa maisha una mvuto na mashiko!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alisema, utakatifu ndiyo sura nzuri zaidi inayopendeza machoni pa walimwengu, changamoto kwa Familia ya Mungu kuhakikisha kwamba, inajikita katika utakatifu wa maisha, kila mtu kadiri ya wito, dhamana na karama yake katika maisha na utume wa Kanisa.

Ikumbukwe kwamba, kila wito unafumbata uzuri na changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi katika hija ya maisha ya kila siku kama sehemu ya mchakato unaotafuta kumwilisha utakatifu wa maisha katika uhalisia wa maisha, Fumbo la Utatu Mtakatifu, likipewa kipaumbele cha kwanza!

Ni changamoto ambayo imetolewa hivi karibuni na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican wakati alipokuwa anashiriki kwenye kongamano la kitaifa kuhusu miito, lililoandaliwa na Baraza al Maaskofu Katoliki Italia, kuanzia tarehe 3 hadi tarehe 5 Januari 2015. Katika mahubiri yake, Kardinali Parolin amewataka waamini kutambua na kuguswa na uzuri huu wenye mvuto unaopania kuwapatia mabadiliko makubwa katika maisha yao, kwa kukutana na Yesu katika Sakramenti, Maandiko Matakatifu, lakini zaidi kati ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Kardinali Parolin anawauliza waamini swali msingi, ikiwa kama kweli wameguswa na Maandiko Matakatifu, kiasi cha kuwachangamotisha kufanya mabadiliko msingi katika maisha yao? Au bado wanaendelea kutangatanga bila ya kuwa na mwelekeo sahihi wa maisha kama "dala dala iliyokatika usukani? Waamini wanapaswa kujenga imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, ili kweli wito na maisha yao yawe ni ushuhuda wa utakatifu unaobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe.

Kardinali Pietro Parolin anasema, haitoshi kwa mwamini kuvutwa na kuguswa na uzuri pamoja na ukweli, lakini wanapaswa kutambua umuhimu wa ujenzi wa mazingira ambamo mambo haya msingi yanaweza kumwilishwa katika uhalisia wa maisha sanjari na kuwashirikisha wengine, pasi na kumezwa na ubinafsi ambao kwa sasa ni kama ugonjwa unaomwandama mwanadamu. Waamini wakati huu wa Kipindi cha Noeli, wamwangalie Mtoto Yesu alivyolazwa kwa unyenyekevu pale Pangoni, huku wakizungukwa na usiku wa giza nene!

Watu wanahitaji kuona cheche za mwanga, ili kutambua kwamba, wanazungukwa na giza nene! Utakatifu ni mwanga angavu katika maisha na utume wa Kanisa, sura yenye mvuto na mashiko!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.