2015-01-05 08:16:41

Watu wamechoshwa na vita, wanataka haki na amani!


Licha ya kinzani, matatizo na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, lakini kuna haja ya kuhakikisha kwamba, makundi yanayopingana nchini humo yanaweka silaha chini, tayari kuanza mchakato wa upatanisho, msamaha na amani inayojikita katika ukweli, uwazi na mafao ya wengi. Kanisa litaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya watu, kamwe halitaogopa wala kunyamazishwa na watu wachache wanaotaka kuvuruga misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa ajili ya mafao yao binafsi.

Ni maneno makali yaliyotolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Afrika ya Kati, aliyetishiwa maisha mara baada ya kutembelea kijiji cha Gbangou, ngome ya kikosi cha waasi cha balaka, ambacho kwa muda wa miaka miwili iliyopita kimeendelea kupandikiza mbegu ya kifo, chuki na uhasama kati ya wananchi. Balaka na Seleka ni makundi makubwa yanayotishia amani na usalama tangu mwezi Machi 2013 baada ya Bozizè kubwaga manyanga baada ya kukumbana na nguvu ya umma iliyomzuia kufanya mabadiliko katika Katiba ya nchi, ili aendelee kukaa madarakani.

Askofu mkuu Nzapalainga anasema, kijiji cha Gbangou kinatisha, watu wanaishi na kutendewa kama wanyama, jambo ambalo kamwe haliwezi kuvumiliwa na wapenda haki na amani duniani, ndiyo maana waliamua kwenda kutembelea na kujionea hali halisi, ili Serikali na Jumuiya ya Kimataifa, iweze kuona kile kinachotendeka huko na hatimaye kuchukua maamuzi machungu. Watu wanaendelea kukabiliana na kifo pole pole kama moto wa kifuu na hakuna mtu anayejali hali kama hii.

Kama mchungaji na mpenda amani, aliamua kwenda kuwatembelea wanakijiji hao ili kuwahakikishia kwamba, hata katika mahangaiko na kilio chao cha damu, bado Mwenyezi Mungu anawapenda na kuwajali, iko siku atawaonesha ile nyota ya matumaini. Askofu pamoja na ujumbe kutoka Caritas Bangui, walifanikiwa kutoa huduma ya tiba kwa wagonjwa waliokuwa wamejikatia tamaa na hivyo wakwafanikiwa tena kuwaonjesha imani na matumaini mapya!

Akiwa njiani, Askofu mkuu Nzapalainga amefanikiwa kukutana na kuzungumza na viongozi mbali mbali wa kidini, kwa kuwataka kuunganisha nguvu na sauti yao, ili kutetea maisha, utu na heshima ya watu wanaoendelea kuteseka kutokana na kinzani pamoja na vita nchini humo. Tangu mwaka 2012, shule nyingi zimeharibiwa kiasi kwamba, watoto na vijana hawana tena fursa ya kuendelea mbele na masomo, ili kuwa na matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.

Watoto na vijana kama hawa wanapaswa kumegewa matumaini, kwa kupatia fursa ya kwenda shule ili kujifunza. Umefika wakati wa kuvuka mipaka ya tofauti zinazowagawa na kuwakinzanisha, ili kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao na ustawi wa wananchi wengi, kuliko tabia ya kuendelea kugubikwa katika chuki, uhasama na ubinafsi uliokomaa kiasi cha kuleta kero na kichefuchefu kati ya watu!

Askofu mkuu Nzapalainga anawataka wahusika wakuu, kuweka silaha pembeni na kuanza mchakato wa majadiliano yanayopania kujenga na kudumisha msamaha, upatanisho wa kitaifa, haki na maendeleo ya wengi. Ni fursa ya kusikilizana katika ukweli na uwazi kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi, kwani haki na amani ni mchakato unaochukua muda mrefu kuweza kuonesha matunda yake, lakini lazima watu waanze kuwajibika. Kila mtu asukumwe na dhamiri safi na nyofu kwa ajili ya kutafuta na kujenga misingi ya haki na amani, ili kufungua ukurasa mpya kwa ajili ya Afrika ya Kati!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.